Diwani Chibago azindua zoezi la ugawaji baiskeli 150 kwa wanafunzi wa Jiji la Dodoma

Na.  Flora   Nadoo, MPUNGUZI

Mwakilishi wa Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Fadhil Chibago amezindua zoezi la ugawaji wa baiskeli 150 kwa wanafunzi wa kike na kiume wanaotembea umbali mrefu kufuata elimu.

Chibago ambae ni Diwani wa Kata ya Dodoma Makulu alizindua zoezi hilo katika Shule ya Sekondari Mpunguzi iliyopo jijini Dodoma.


Mwakilishi wa Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Fadhil Chibago akimkabidhi mmoja wa wanafunzi wa Shule ya Sekondari Mpunguzi baiskeli


Diwani Chibago alisema “zoezi hili linahusisha ugawaji wa baiskeli 150 katika shule tano za sekondari za Mkoa wa Dodoma. Baiskeli hizi ili ziishi ni lazima sisi tuzitunze. Hivi si vyombo ambavyo ni kamili, haviwezi kuharibika, vitaharibika. Lakini je ni sahihi kwamba baiskeli ikiwa imepata pancha irudishwe? Jibu ni hapana, kwa sababu hii haijakaa sawa, yale matatizo madogo madogo tunaweza kuyatatua wenyewe. Hivyo, basi kuna msemo unaosema kuwa ukibebwa na wewe bebeka. Shirika hili wanafanya kazi nzuri sana na sisi tuwatie moyo kwa kutatua matatizo madogo madogo ambayo yatakuwa yanajitokeza kama vile pancha. Programu hii ni nzuri sana kwa sababu inaonesha ni namna gani mashirika binafsi ambavyo yanaunga mkono jitihada za serikali za kusaidia wanafunzi wote waweze kupata elimu, siyo kupata elimu tu bali kuwasaidia kuweza kufika shuleni kwa wakati, ambacho ni kitu kizuri” alisema Chibago.

Kwa upande wa Meneja Mradi wa Shirika la ABC Impact, Mohamed Musa alisema kuwa programu hiyo ilianzishwa mwaka 2022 na ndio ilisajiliwa na tukapata cheti kutoka Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Wenye Ulemavu na tulipata kibali kutoka TAMISEMI. “Kwahiyo, tuko kihalali kabisa na tunafanya hizi kazi kuanzia mwaka 2022. Mpaka leo, tumegawa baiskeli karibu 3,200, tunafanya kazi mikoa mitano kwenye shule zaidi ya 50. Tunafanya hii kazi ya kuhudumia jamii sana na tuna uzoefu huo. Baiskeli hizi haziuzwi ila tumeamua kuweka kigezo hiki makusudi cha mtu kuchangia nauli kufika hapa. Nauli yenyewe ni shilingi 38,000. Baiskeli hizi anazinunua mdau anayeitwa Veraafrika yuko Switzerland, anatuwezesha sisi kama shirika kwaajili ya kuwasaidia wanafunzi ambao wanauhitaji” Mussa.

Pia aliendelea kusema kuwa shirika hilo linahusisha mikoa sita ambayo ni Arusha, Dodoma, Kilimanjaro, Manyara, Mwanza na Shinyanga. “Baiskeli tulizogawa kwa watu ni jumla ya baiskeli 3,200. Zoezi hili linahusisha ugawaji wa baiskeli 150 katika shule za sekondari tano za Mkoa wa Dodoma. Wanufaika wa baiskeli hizi ni wanafunzi wa kike na wa kiume wanaotembea umbali mrefu kwenda na kurudi shuleni ili kutatua changamoto ya kutembea umbali mrefu. Ningependa kutaja faida za baiskeli kwa wanufaika, kwanza ni kuongeza muda wa mwanafunzi kufanya shughuli za ziada, inapunguza idadi ya wanafunzi kuacha shule, inasaidia wanafunzi kuacha utoro, inamsaidia mwanafunzi kujiamini pia inasaidia kutimiza ndoto za mwanafunzi. Hivyo, basi hapa Mpunguzi tumeleta baiskeli 70 mpaka sasa. Shule ambayo tumegawa baiskeli 150 ni shule tano ambapo kila shule baiskeli 30. Shule ya kwanza ni Mpunguzi, Chihanga, Mtemi Chiloloma, Mbalawala na Chibelela.


Mwakilishi wa Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Fadhil Chibago akikata utepe kuashiria uzinduzi wa zoezi la ugawaji wa baiskeli


Nae Diwani wa Kata ya Mpunguzi, Innocent Nyambuya alimshukuru mgeni rasmi, walimu, wazazi na wanafunzi kwa kuhudhuria katika uzinduzi huo. Pia alilishukuru Shirika la ABC_Impact kwa msaada wao walioutoa kwa wanafunzi. Alisema “namshukuru sana Mungu kwa hili Shirika la ABC_Impact ambalo limetusaidia sisi kama serikali kwa kuwagusa wanafunzi wanaotoka umbali mrefu kuja kuifuata elimu” alisema Nyambuya.

Afisa Alimu Kata ya Matumbulu, Ally Mgoo alisema kuwa ugawaji wa baiskeli hizo utawarahisishia wanafunzi kuwahi vipindi shuleni. “Kwa upande wetu, idara ya elimu tunashukuru sana kwa msaada uliotolewa na Shirika la ABC Impact. Msaada huu unaenda kuwa chachu kwa maendeleo ya wanafunzi wetu. Moja ya maendeleo ambayo tunategemea kuyapata ni ufaulu mzuri kwa sababu wanafunzi watakuwa wanawahi vipindi vyao kila siku. Pia vishawishi kwa waendesha bodaboda vitapungua kwa wanafunzi. Ombi letu sisi kama idara tunaomba mashirika mengine yaige mfano kwa Shirika la ABC Impact” alisema Mgoo.

Kwa upande wake Mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Mpunguzi, Musa Abdallah alitaja faida za baiskeli hizo. “Baiskeli zitaimarisha viungo, kuwahi vipindi na kuwahi kurudi nyumbani” alisema Abdallah.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma