Shilingi Bilioni 1.5 kujenga Hospitali ya Wilaya Dodoma

 Na. Dennis Gondwe, DODOMA

SERIKALI imetoa shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Dodoma katika jitihada za kusogeza huduma bora za afya karibu zaidi na wananchi.

Moja ya majengo ya Hospitali ya Wilaya ya Dodoma


Kauli hiyo ilitolewa na Mkuu wa Divisheni ya Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Dkt. Andrew Method alipokuwa akiongelea mafanikio ya serikali ya awamu ya sita kwa kipindi cha miaka mitatu kwa waandishi wa habari ofisini kwake jijini hapa.

Dkt. Method alisema “tunapoongelea mafanikio ya serikali ya awamu ya sita kwa kipindi cha miaka mitatu, mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa fedha shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Dodoma. Na hiyo hospitali ya wilaya ipo kimkakati kabisa, inajengwa eneo la Kata ya Nala. Ni eneo ambalo linaweza kufikiwa na rufaa ya vituo vyote vya afya ambavyo vinapitiwa na barabara ya mzunguko ‘ring road’. Kwa hiyo utaona hii barabara ya mzunguko inaenda kusaidia hadi utoaji wa huduma za afya kwa wananchi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma. Wagonjwa wakipewa furaa watapika katika barabara ya mzunguko kwenda hospitali ya wilaya na kuweza kupatiwa huduma. Hospitali hii ipo katika hatua ya umaliaziaji kwa sababu ujenzi wake umefikia asilimia 80. Matarajio yetu mwezi Julai mwaka huu ianze kutoa huduma katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma”.

Akiongelea majengo yanayojengwa, aliyataja kuwa ni maabara, jengo la wagonjwa wa nje na jengo la mama na mtoto. Majengo mengine ni jengo la mionzi, jengo la dawa, jengo la kuhifadhi maiti na kichomea taka.  

Mkuu wa Divisheni ya Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe, Dkt. Andrew Method


Wakati huohuo, alisema kuwa serikali ya awamu ya sita imeendea kuboresha miundombinu ya Kituo cha Afya Makole. “Mheshimiwa Rais, hakuishia kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Dodoma, ametoa shilingi milioni 750 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la ghorofa nne ambalo litatoa huduma katika Kituo cha Afya Makole. Kama mnavyofahamu kituo hiki ni kikongwe na kinahudumia wananchi takribani 600 kwa siku” alisema Dkt. Method.

Ikumbukwe kuwa Halmashauri ya Jiji la Dodoma ina jumla ya vituo 44 vya kutolea huduma, kati ya hivyo, vituo 38 ni zahanati na sita ni vituo vya afya ikiwa na wakazi wapatao 765,179. Huduma za afya ngazi ya wilaya wamekuwa wakizipata katika Hospitali ya Mtakatifu Gemma iliyopo Kata ya Miyuji.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma