Marufuku mifugo kuzurura Kata ya Mnadani

Na. Dennis Gondwe, MNADANI

WAFUGAJI wa Kata ya Mnadani wametakiwa kuacha tabia ya kuzurulisha mifugo yao na kufanya ufugaji wa ndani ili kwenda sambamba na mahitaji ya hadhi ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma.



Kauli hiyo ilitolewa na Afisa Mifugo wa Kata ya Mnadani, Elizabeth Shirima alipokuwa akiongea na mamia ya wananchi wa Mtaa wa Mnadani katika mkutano wa hadhara.

Shirima alisema kuwa kata hiyo inakabiliwa na ufugaji holela. “Mifugo inayozuzura ovyo ni ile ya ufugaji huria, Dodoma sasa ni Jiji hivyo, hakuna utaratibu wa kuzurulisha mifugo hasa katika barabara za lami na mitaa. Naomba wafugaji kama hamuwezi kufugia ndani mnashauriwa kuhamisha mifugo kutoka Jiji kwenda maeneo yanayokubalika hasa ufugaji wa wanyama wakubwa kama ng’ombe, mbuzi, punda, na ngamia. Kuna wakati gari la kubeba wagonjwa linakimbiza mgonjwa hospitali inabidi lisimame kusubiri mifugo ipite barabara kuu. Halmashauri ya Jiji imetenga maeneo kwa ajili ya wafugaji. Unapohitaji kununua eneo la kufuga mifugo nenda Ofisi ya Halmashauri ya Jiji kwa ajili ya kununua eneo la kufuga mifugo kwa mujibu wa Mpango Kabambe wa halmashauri” alisema Shirima.

Afisa Mifugo huyo alitoa tahadhari ya msimu wa mvua kwa mifugo. “Msimu huu wa mvua kuna kuwa na uibukaji wa magonjwa kwa mifugo. Tunahimiza wafugaji kuogesha mifugo yenu. Pia unapoona changamoto kwa mifugo yako toa taarifa mapema ili tushughulike mapema” alisema Shirima.

Kwa upande wake Afisa Mtendaji Mtaa wa Mnadani, Njuu Mpangala aliwataka wananchi wa mtaa huo kuwa na tabia ya kuhudhuria mikutano ya hadhara. “Mheshimiwa Mwenyekiti, yale tuliyokubaliana tukayatekeleze, kuyasimamia na kuhakikisha mtaa wetu unanyooka. Wale wote ambao hawakuja katika mkutano huu wapeni hizi taarifa mlizopata hapa. Mwingine akikamatwa na kupigwa faini asiseme hakufahamu tuliyokubaliana katika mkutano. Pia jengeni tabia ya kuwa mnahudhuria mikutano hii tunapoiitisha ni sehemu ya ushirikishanaji mipango ya maendeleo ya mtaa wetu na ndiyo demokrasia inavyotaka” alisema Mpangala.

 

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Osterbay Dodoma wajitokeza usafi wa mazingira

Usafi wa Mazingira Kipaumbele Kata ya Chamwino

Wananchi wa Kata ya Mtumba wanufaika na Mikopo ya asilimia 10 ya Halmashauri