Vikundi vyapatiwa Mil. 215 Kata ya Mnadani

 Na. Dennis Gondwe, MNADANI

VIKUNDI ya wanawake vijana na watu wenye ulemavu 18 vimepata mikopo ya shilingi 215,000,000 katika kipindi cha kuanzia mwaka 2021 hadi mwaka 2023 katika Kata ya Mnadani.

Picha kutoka maktaba ya Jiji la Dodoma


Takwimu hiyo ilitolewa na Afisa Mtendaji Kata ya Mnadani, Caroline Massawe alipokuwa akiwasilisha taarifa ya mafanikio ya serikali ya awamu ya sita kwenye mkutano wa hadhara wa wananchi wa Mtaa wa Mnadani.

Massawe alisema kuwa sekta ya maendeleo ya jamii imepiga hatua kubwa katika kipindi cha miaka mitatu na kuwainua wananchi wa kata hiyo. “Kuanzia mwaka 2021 hadi sasa katika Kata ya Mnadani, vikundi 18 vimepata mikopo na shilingi 215,000,000 zimetolewa. Kati ya vikundi hivyo, vikundi sita ni vya wanawake vilivyokopeshwa shilingi 49,000,000. Vikundi tisa vya vijana vimekopeshwa shilingi 142,000,000 na vikundi vitatu vya watu wenye ulemavu vimekopeshwa shilingi 24,000,000 na kufanya jumla ya shilingi 215,000,000. Mikopo hii imekuwa na manufaa sana kwa wananchi wetu kwa sababu imewaongezea mtaji na kuwakwamua kiuchumi” alisema Massawe.

Wakati huohuo, aliwataka wazazi kukaa na watoto wao na kuwapa elimu dhidi ya masuala ya ukatili wa kijinsia. “Kata ya Mnadani tumefanya ziara kadhaa katika shule kutoa elimu dhidi ya madhara ya ukatili wa kijinsia kwa watoto. Ndugu zangu hali siyo shwari, watoto wadogo wanafanyiwa ukatili. Wazazi kaeni chini na watoto wenu kutoa elimu dhidi ya ukatili wa kijinsia. Watoto wanafahamu mambo makubwa kulikoa tunavyofikiria” alisema kwa uchungu.

Kwa upande wake Afisa Mtendaji Mtaa wa Mnadani, Njuu Mpangala aliwataka wananchi wa mtaa huo kuwa na tabia ya kuhudhuria mikutano ya hadhara. “Mheshimiwa Mwenyekiti, yale tuliyokubaliana tukayatekeleze, kuyasimamia na kuhakikisha mtaa wetu unanyooka. Wale wote ambao hawakuja katika mkutano huu wapeni hizi taarifa mlizopata hapa. Mwingine akikamatwa na kupigwa faini asiseme hakufahamu tuliyokubaliana katika mkutano. Pia jengeni tabia ya kuwa mnahudhuria mikutano hii tunapoiitisha ni sehemu ya ushirikishanaji mipango ya maendeleo ya mtaa wetu na ndiyo demokrasia inavyotaka” alisema Mpangala.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma