WIZARA YA ARDHI KUBORESHA MFUMO WA ILMIS

 Na. Dennis Gondwe, DODOMA

WIZARA ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi inaendelea kuboresha mfumo wa kieletroniki wa kutunza taarifa za Ardhi (ILMIS) ili kuboresha utoaji wa huduma ikiwemo kurahisisha upatikanaji wa hati milki ikiwa niutekelezaji maelekezo ya serikali.

Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Jerry Slaa akiongea na waandishi wa habari


Kauli hiyo ilitolewa na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Jerry Slaa alipokuwa akiongea na waandishi wa habari leo katika Ofisi ya Ardhi Mkoa wa Dodoma kuhusu utekelezaji wa maelekezo ya serikali kuhusu kuboresha huduma za sekta ya Ardhi katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma na Mwanza.

Slaa alisema “tarehe 3 Oktoba, 2023 serikali ilitoa maelekezo mbalimbali yaliyolenga kuboresha huduma za sekta ya Ardhi katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma na Mwanza. Maelekezo hayo yalihusu mamlaka mbalimbali zinazohusika na usimamizi wa sekta ya Ardhi. Wizara inaendelea na uboreshaji wa mfumo wa kieletroniki wa kutunza taarifa za Ardhi ili kuboresha utoaji wa huduma ikiwemo kurahisisha upatikanaji wa hati milki na utoaji huduma kwa wananchi kwa njia ya mtandao. Maboresho yay a mfumo huu yatakamilika mwishoni mwa mwaka huu 2023 na kusambazwa nchi nzima”.

Eneo lingine alilitaja kuwa ni tathmini ya awali kubaini madai ya viwanja mbadala 3,992. “Halmashauri ya Jiji la Dodoma imekwishabainisha viwanja 1,102 vilivyopo maeneo ya Nala Lugala (1,035) na Mkonze (97) kwa ajili ya fidia na baadhi ya wananchi wameanza kupewa. Aidha, Halmashauri ya Jiji la Dodoma inaendelea na upimaji wa viwanja 5,000 katika eneo la Mahomanyika ambavyo vitatumika kufidia wananchi wenye madai” alisema Slaa.
Maelekezo mengine aliyataja kuwa ni wizara yake kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa imetoa maelekezo ya kuhuisha kamati za ugawaji Ardhi katika ngazi husika katika ugawaji wowote unaofanyika. “Kuzingatia Sheria za Ardhi na Waraka wa Waziri Na. 1 katika ulipaji fidia ambao unasisitiza kutenga fedha za kulipa fidia kabla Mthamini Mkuu hajaidhinisha majedwali ya kulipa fidia. Kumilikisha na kulinda maeneo ya serikali na kuweka alama za kudumu zinazoonekana” alisisitiza Slaa.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma