BANDA YA JIJI LA DODOMA LATOA TEKNOLOJIA UFUGAJI SAMAKI NA KUKU PAMOJA

Na. Dennis Gondwe, NZUGUNI

WANANCHI wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma wamehamasishwa kujifunza teknolojia ya ufugaji wa samaki na kuku kwa pamoja ili kujiongezea kipato.

Afisa Uvuvi katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Tausi Kiula


Hamasa hiyo ilitolewa na Afisa Uvuvi katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Tausi Kiula alipokuwa akihamasisha ufugaji wa pamoja wa samaki na kuku kwa wananchi waliotembelea banda la mifugo la Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Kiula alisema “tunawahamasisha wananchi wote waje wajifunze katika bwawa letu hapa. Kama unavyoona teknolojia nzuri ya kisasa ambayo unapoiona unahamasika. Unachimba bwawa la samaki kisha unajenga kibanda cha kuku kwa juu yake ili kuku wakiwa wanajisaidia kinyesi kinadondoka katika bwawa la samaki na kusaidia ‘fertilization’ kwa kuweka mbolea inayobadilisha maji kuwa ya kijani na kutengeneza chakula cha samaki”.

Akiongelea umuhimu wa ufugaji huo alisema kuwa unawahakikishia samaki chakula bora. “Maji yanapobadilika kwenda rangi ya kijani, ule ukijani maana yake ni mimea inajitengeneza kutokana na ile mbolea ambayo ni kinyesi cha kuku na inatumika kama chakula cha samaki. Pia ufugaji huu unampatia kipato mfugaji kwa wakati mmoja kutokana na bidhaa mbili yaani kuuza samaki na kuku kwa pamoja. Pia matumizi binafsi kama kitoweo” alisema Kiula.

Kuhusu aina ya bwawa linaloshauriwa, alisema kuwa linatakiwa kuwa na mteremko na sehemu ya kuingilia maji inayokuwa kwenye kina kifupi na sehemu ya kutolea maji inayokuwa kwenye kina kirefu. “Ili kufuga samaki kisasa mfugaji anashauriwa baada ya wiki mbili awe anasafisha bwawa lake kwa kupunguza maji na kuongeza maji mengine masafi” alisema Kiula.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma