JIJI LA DODOMA KUPELEKA MIL 50 ZAHANATI YA KIKUYU

Na. Dennis Gondwe, KIKUYU KASKAZINI

SERIKALI kupeleka shilingi milioni 50 kukamilisha jengo la wodi ya wazazi katika Zahanati ya Kikuyu iliyopo Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa lengo la kuwafikishia huduma za afya wananchi.

Mbunge Anthony Mavunde


Kauli hiyo ilitolewa Mbunge wa Jimbo la Dodoma mjini, Anthony Mavunde alipokuwa akiongea na mamia ya wananchi wa Kata ya Kikuyu Kaskazini waliojitokeza kushiriki zoezi la usafi wa mazingira na upandaji miti kuzunguka Zahanati ya Kikuyu.

Mavunde alisema “Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya ya Dodoma jengo unaloliona kushoto kwako ni jitihada zangu mimi na diwani wa hapa. Habari njema ni kwamba kabla ya Jumatano wiki ijayo tunaingiza shilingi milioni 50 ambazo zitakwenda kukamilisha jengo hilo. Na nategemea mwezi Oktoba mwaka huu kina mama wataanza kuhudumiwa katika wodi ya wazazi”.

Akiongelea historia ya jengo hilo, alisema kuwa mwaka 2020 aliwaahidi wananchi wa kata hiyo kujengewa wodi ya wazazi. “Nilikuja hapa nikiwa na Diwani Mwansasu nikakuta kina mama wanahudumiwa hapo kwenye korido, sehemu ambayo haikuwa na staha kwa mama zetu, nikamwambia Daktari nitahakikisha tunajenga jengo la kina mama. Nimemuomba Daktari anisaidie kupata ramani ya hapa ili tuone mipaka. Kwa uzuri wa zahanati yetu na mazingira yake tutaanza kujichanga tuweke uzio kwenye zahanati yetu” alisema Mavunde kwa furaha ya mandhari za zahanati hiyo.

Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Jabir Shekimweri aliyekuwa kinara katika zoezi la kupanda miti na usafi wa mazingira katika kata hiyo aliungana na mbunge kuipongeza Zahanati ya Kikuyu kwa wazo la kuboresha mandhari yake. “Ni dhamira yetu tutafute ‘model’ ya uangalizi wa mazingira katika maeneo yetu ya kutolea huduma ya afya katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma. “Tumekubaliana hilo paa hapo halipendezi kwa hiyo tulipake tu rangi nyekundu ili liweze kupendeza harafu kituo kirudishiwe rangi ya njano ndiyo rangi ya eneo hili Mheshimiwa Mbunge. Mbunge amening’ata sikio hilo la kubadilisha paa isiwe la kupaka rangi yeye atatuletea mabati mapya” alisema Shekimweri huku akitabasamu.

Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Jabir Shekimweri akiongea na wananchi


Akiwahakikishia wananchi wa Kikuyu Kaskazini kukamilika kwa jengo la wazazi katika zahanati hiyo alisema kuwa serikali italikamilisha. Mheshimiwa Mbunge unafahamu fedha za kuboresha zahanati hii ni matokeo ya bakaa kwa mwaka wa fedha ulio kwisha. Hivyo, jengo hilo tutalikamilisha” alisema.

 

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma