AFISA MTENDAJI KATA YA CHAMWINO APEWA CHETI UTEKELEZAJI MKATABA WA LISHE JIJI LA DODOMA

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

AFISA Mtendaji wa Kata ya Chamwino, Lucas Nkelege amepongezwa na kupatiwa cheti kwa kufanya vizuri katika utekelezaji wa Mkataba wa Lishe katika jijini Dodoma.

Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Jabir Shekimweri akimkabidhi cheti kutambua kazi nzuri ya utekelezaji Mkataba wa Lishe Afisa Mtendaji Kata ya Chamwino, Lucas Nkelege


Pongezi hizo zilitolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya Lishe Wilaya ya Dodoma, Jabir Shekimweri alipoongoza Kikao cha Tathmini ya Mkataba wa Lishe kwa robo ya nne kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Shekimweri ambae ni Mkuu wa Wilaya ya Dodoma alisema kuwa suala la lishe ni muhimu kwa wilaya yake na maafisa watendaji wa kata wana wajibu wa kusimamia lishe katika maeneo yao. “Ndugu zangu, napenda kuwaambia tunatakiwa kuwa na tafsiri pana na dhamira ya Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhusiana na suala la lishe. Tuhakikishe watoto wanapata chakula shuleni. Wale wote ambao hatujafanya vizuri kwenye “score card” katika kipengele cha chakula shuleni, niwaombe mkafanye tathmini ya kina na kuweka mikakati mahususi na nipate taarifa ya utekelezaji wa mikakati hiyo. Aidha, mikakati hiyo iwasilishwe kwa waratibu wa lishe. Waratibu wa lishe muandae timu ya kufuatilia ‘site’ kuangalia mikakati inavyotekelezwa. Nipo tayari na nitakuja kwenye maeneo ambayo watu wapo tayari na wamejitoa, nije kuwaongezea nguvu. Siyo nguvu ya maneno tu bali ya vitendo na uwezeshaji ili chakula kipatikane shuleni”.

Mkuu wa Wilaya ya Dodoma akisisitiza umuhimu wa Lishe kwa jamii


Akiongelea umuhimu wa cheti cha pongezi, Afisa Mtendaji wa Kata ya Chamwino, Lucas Nkelege alisema kuwa amehamasika zaidi kutekeleza Mkataba wa Lishe katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma. “Cheti hiki ambacho kinatambua mchango wangu kufanya vizuri katika utekelezaji wa Mkataba wa Lishe kimenipa motisha. Nimepata motisha zaidi ya kutekeleza majukumu ya lishe. Mfano kufanya maadhimisho ya Siku ya Afya na Lishe kwa mitaa na jamii kwa ujumla. Aidha, nimepata hamasa ya kuendelea kuhamasisha lishe katika shule ili kuhakikisha wanafunzi wanapata chakula na kutoa elimu ya lishe katika ngazi ya mtaa ili kutokomeza hali ya udumavu na utapiamlo kwa watoto” alisema Nkelege.

Kwa upande wake Afisa Lishe wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Semeni Juma alisema kuwa kikao hicho kinafanya tathmini ya robo ya nne na nusu mwaka ya mkataba wa Lishe. “Kwa kuwa tumemaliza mwaka wa fedha 2022/2023, tunafanya tathmini ya mwaka mzima kuona kiutekelezaji mkataba huu wa lishe tumeutekeleza kwa kiasi gani ili kujipanga vizuri zaidi kwa utekelezaji mwaka ulioanza” alisema Juma.

 


MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma