Madiwani Jiji la Dodoma wasisitizwa kufanya kazi kwa weledi na ushirikiano

Na. Mwandishi Wetu, DODOMA

Madiwani wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma wapongezwa kwa kuaminiwa na wananchi na kutakiwa kufanya kazi kwa uwajibikaji, ushirikiano na weledi wa hali ya juu.



Hayo aliyasema Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaji. Jabir Shekimweri wakati wa mkutano wa kwanza wa Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma uliofanyika katika ukumbi wa halmashauri.

Alisema kuwa anawataka madiwani kuimarisha uwazi na uwajibikaji katika utendaji wao, kusikiliza kero za wananchi na kuhakikisha kuwa mipango ya maendeleo inalenga kuleta manufaa kwa jamii nzima. “Dodoma kama makao makuu ya nchi inahitaji uongozi thabiti, wa mfano na wenye matokeo. Ni wajibu wenu kuhakikisha jiji linaendelea kuwa kioo cha maendeleo kwa taifa hasa kwa kuibua miradi yenye tija kwa wananchi na kuwapa kipaumbele zaidi wananchi kwa kusikiliza kero zao” alisema Shekimweri.

Aidha, alisisitiza umuhimu wa madiwani kushirikiana na watendaji wa halmashauri katika kutekeleza miradi ya maendeleo, kuboresha huduma za kijamii na kusimamia ipasavyo matumizi ya rasilimali za umma. “Serikali inatarajia kuona mabadiliko chanya katika maeneo yote ya jiji, hususan katika miundombinu, usafi, ukusanyaji wa mapato na utawala bora, haya yote yatatokea pale amabapo kutakuwa na ushirikiano mzuri baina yenu na watendaji, hatutarajii kusikia kero ya aina yoyote inayohusu Afisa Mtendaji wa Kata. Hivyo, nendeni mkafanye kazi kwa ushirikiano na kuwapa kipaumbele wananchi” alisema Shekimweri.


Kwa upande wake, Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma, Alimwoni Chaula, alimshukuru mkuu wa wilaya kwa mwongozo wake na kuahidi kushirikiana kikamilifu na serikali pamoja na wananchi katika kutekeleza majukumu yao. “Kwanza nipende kumshukuru mkuu wa wilaya kwa kutukumbusha majukumu yetu, lakini sisi kwa kushirikiana na serikali tutakwenda kuimarisha huduma za kijamii, kuongeza ufanisi wa utendaji wa halmashauri na kuharakisha maendeleo ya Jiji la Dodoma. Pia kupitia uongozi wangu utaongozwa na misingi ya uwazi, ushirikishwaji na nidhamu katika matumizi ya rasilimali za umma” alisema Chaula.


MWISHO

 

 

Comments

Popular Posts

Agenda ya Lishe yaongeza Ari ya usomaji S/M Dodoma Makulu

Miaka minne ya Dkt. Samia, Kizota yanufaika mikopo ya asilimia 10

Halmashauri ya Jiji la Dodoma Kuhudumia Majimbo Mawili ya Uchaguzi