DC Shekimweri aongoza mazoezi ya Kilomita 5

 

 Na. Mwandishi Wetu, DODOMA

Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri apongeza Umoja wa Klabu za Mbio za Pole kwa kujitokeza na kuhamasisha upimaji wa afya na matibabu bure kwa magonjwa yasiyoambukiza.

 


Mbio hizo zilianzia katika Ofisi ya Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma na kuhitimishwa katika bustani ya mapumziko Nyerere Square ambapo maadhimisho hayo ya Wiki ya Upimaji Magonjwa yasiyoambukiza yalitamatika.

Alisema kuwa anawashukuru waandaji wa kliniki hiyo kwa kutoa huduma bora. “Siku ya kwanza walipokea wananchi 450 waliojitokeza kupata vipimo na matibabu, jana walihudumia wananchi zaidi ya 300. Kwahiyo, kwa ujumla wamehudumia jumla ya wananchi 1,500. Nimefurahi sana kusikia mwitikio ni mkubwa pia ni imani yetu kuwa baada ya zoezi hili kutamatika, tutafanya upembuzi ili kuona namna tunaweza kufanya zoezi hili kuwa endelevu tukihusishanisha na mazoezi’’ alisema Alhaj Shekimweri.

Pia aliwashukuru wananchi wote waliofuatilia Hotuba ya Rais Dkt. Samia wakati akizindua Bunge. “Mheshimiwa rais alizungumza mambo mengi yaliyowapa matumaini wananchi na akaeleza msimamo wa serikali kwa jumuia za kimataifa. Lakini kubwa zaidi hotuba ile ilizungumzia sana vijana na kwasababu karibia kundi kubwa zaidi hapa nchini ni vijana hilo lilikuwa jambo jema” alishukuru Alhaj Shekimweri.

Alhaj Shekimweri alimalizia kwa kuwaasa wananchi na wahudhuriaji wa mbio hizo kuzingatia lishe bora ili kujenga mwili imara. “Ndugu zangu, tukishirikiana katika kuhamasisha ulaji mzuri wa vyakula, tutafukuza maradhi mengi. Sisi hapa tuwe mfano wa kuhamasisha jamii kwasababu gharama za matibabu ni kubwa sana, hizo gharama za kujihudumia zingeelekezwa kwenye miradi ya maendeleo kwa ngazi ya familia na Taifa kwa ujumla” alimaliza.

Nae, Mganga Mkuu wa Jiji la Dodoma, Dr. Pima Sebstian aliwashukuru wananchi kwa kuonesha mwitikio mzuri kwa kujitokeza kupata huduma ya matibabu ya awali na kujua afya zao. “Tunawashukuru wananchi wote waliojitokeza kupata huduma katika wiki ya maadhimisho ya magonjwa yasiyoambukiza. Tuendelee kupambana na mtindo wa maisha ili kuyaondoa maradhi haya ambayo yamekuwa tishio, tuendelee kuzingatia ushauri wa madaktari kwasababu maelekezo tunayotoa yanatekelezeka” alishukuru.

Kwa upande wake Katibu wa Dodoma Jogging Association, Swalihina Ally alisema kuwa mazoezi ya mbio za pole ni sehemu muhimu ya kuboresha afya na kufukuza maradhi yanayoepukika. Aliwaasa wananchi kufanya mazoezi kwa wingi na kuzingatia lishe bora ili kuwa katika uwiano sawa wa afya njema.

Katika hatua nyingine, Afisa Michezo Jiji la Dodoma, Neema Kilongola amewapongeza wanamichezo kwa kujitokeza kwa wingi katika mazoezi hayo yanayohamasisha utunzaji wa afya. “Maadhimisho ya wiki ya upiamji magonjwa yasiyoambukiza yameonesha mwamko mkubwa wa wananchi kujitokeza kupima afya, ni jambo jema na tunawapongeza kwa hilo. Pamoja na hayo, tunawakumbusha kupenda mazoezi na kuzingatia lishe bora, tuachane na tabia bwete ili kuimarisha afya zetu na kuyaondoa maradhi yanayozuilika kwa kuwa na mtindo mzuri wa maisha” alipongeza.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Agenda ya Lishe yaongeza Ari ya usomaji S/M Dodoma Makulu

Miaka minne ya Dkt. Samia, Kizota yanufaika mikopo ya asilimia 10

Halmashauri ya Jiji la Dodoma Kuhudumia Majimbo Mawili ya Uchaguzi