Wasimamizi Wasaidizi Uchaguzi wapewa Semina Dodoma

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

Wasimamizi wasaidizi wa uchaguzi ngazi ya kata wametakiwa kusoma katiba, sheria na miongozo inayotolewa na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa weledi na kufanikisha Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani.


Msisitizo huo ulitolewa na Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Dodoma Mjini na Mtumba, Wakili Cosmas Nsemwa wakati akifungua mafunzo kwa wasimamizi wasaidizi wa uchaguzi ngazi ya kata yaliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Alianza kwa kuwapongeza washiriki wa mafunzo kwa kuteuliwa kuwa wasimamizi wasaidizi wa uchaguzi ngazi ya kata. “Someni kwa umakini katiba, sheria, kanuni, miongozo na maelekezo mbalimbali yaliyotolewa na yatakayotolewa na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi na ulizeni maswali ili mpate kufafanuliwa kwenye maeneo ambayo kwa namna moja au nyingine pengone yatakuwa na changamoto za kufahamu ili kuwarahisishia katika utekelezaji wenu wa kazi za uchaguzi” alisema Wakili Nsemwa.

 Msimamizi huyo wa uchaguzi aliwasisitiza washiriki kuvishirikisha vyama vyote vya siasa vyenye usajiri kamili katika hatua zote kwa kuzingatia matakwa ya katiba, sheria, kanuni na maelekezo ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi. “Washirikisheni wadau wa uchaguzi hususan katika maeneo ambayo kwa mujibu wa katiba, sheria, kanuni, miongozo na maelekezo mbalimbali yanayotolewa na yatakayotolewa na Tume ambao wanastahili kushirikishwa” aliongeza.



Maeneo mengine aliyosisitiza kwa wasimamizi wasaidizi hao ni kujiepusha kuwa vyanzo vya malalamiko kutoka kwa vyama vya siasa na wadau wa uchaguzi. Aidha, aliwataka kuzimatia katiba, sheria, kanuni, miongozo na maelekezo yanayotolewa na Tume. “Fanyeni utambuzi wa vituo vya kupigia kura mapema ili kubaini mahitaji maalum ya vituo husika na kuhakikisha kunakuwa na mpangilio mzuri ambao utaruhusu uchaguzi kufanyika kwa utulivu na amani. Hakikisheni vifaa vya uchaguzi mnavipokea kutoka Tume, mnavihakiki, mnavikagua na kuhakikisha vinasambazwa kwenye vituo vyote na kila mkuu wa kituo anapata vifaa vyote vya uchaguzi vinavyohitajika mapema” alisisitiza Wakili Nsemwa.

Wakati huohuo, aliwakumbusha wasimamizi wasaidizi hao wa uchaguzi ngazi ya kata kufanya kazi kwa weledi na kujituma. “Dhamana mliyopewa ya kusimamia na kuratibu uendeshaji wa uchaguzi wa Rais na wabunge wa Jamhuri ya Muungano na madiwani kwa Tanzania bara ni kubwa, nyeti na muhimu kwa mustakabali wa taifa letu. Hivyo, mnategemewa kuzingatia utendaji wenu, muwajibike ipasavyo katika kipindi chote cha utumishi wenu kwa Tume hadi tutakapokamilisha jukumu hili la uchaguzi mkuu” alisisitiza Wakili Nsemwa.

Awali akimkaribisha mgeni rasmi kufungua mafunzo hayo, Mwenyekiti wa mafunzo, Tunu Dachi alimuhakikishia mgeni rasmi kuwa nafasi waliyopewa washiriki wa mafunzo hayo wataitengea haki. “Tunamuomba Mwenyezi Mungu atupe kibali mwanzo hadi mwisho tufanikishe uchaguzi mkuu” alisema Dachi.



Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Uchaguzi Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Albert Kasoga alimtaarifu mgeni rasmi kuwa mafunzo hayo ya siku tatu yanahusisha washiriki 82 kutoka katika kata 41. Alimuhakikishia kuwa washiriki wa mafunzo hayo wanaendelea kuwa bora kila kukicha na kusema kuwa baada ya mafunzo hayo watakuwa bora zaidi.

Wasimamizi wasaidizi wa uchaguzi ngazi ya kata waliteuliwa kwa kuzingatia masharti ya kifungu cha 6(2) cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na. 1 ya mwaka 2024 na katika mafunzo hayo jumla ya mada 11 zitawasilishwa na kujadiliwa kwa kina.




MWISHO

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

RC Dodoma apongeza wafugaji kwa ushiriki wa Paredi ya Mifugo

Rais Samia: Tumieni kikamilifu Miundombinu, Teknolojia na mitaji iliyowekezwa katika Kilimo, Uvuvi na Mifugo