Kilimo cha Mbogamboga kukuza Afya na kipato kwa wananchi Jiji la Dodoma

Na. Eupilio Anthony, DODOMA

Mamia ya wananchi wameonesha hamasa kubwa kutembelea mabanda ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma yenye teknolojia mpya za kilimo, mifugo bora, ufugaji wa kisasa wa samaki, pamoja na bidhaa za viwandani zinazotengenezwa na wajasiriamali wa ndani kutokana na mazao ya kilimo na mifugo katika maonesho ya Nanenane.

Kauli hii ilitolewa na Afisa Kilimo Mwandamizi Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Nkunde Kimweri alipozungumza na waandishi wa habari waliofika kwenye banda la kilimo cha mbogamboga upande wa bustani kwenye maonesho ya wakulima Nanenane Nzuguni jijini Dodoma.

Alisema kuwa kilimo cha kisasa cha mbogamboga kina njia nyingi za kukifanya kiwe na faida kwa afya na kiuchumi. “Hapa tunakipando cha bustani kichuguu ambacho tumepanda mboga mbalimbali, tuna mboga tofauti tofauti ambazo tunazitumia nyumbani. Kwa sasa tunahamasisha wananchi kulima mboga mboga hata kwenye maeneo madogo ya nyumbani kwao, kwa kutumia vichuguu kwasababu ni njia rahisi na safi sana. Pia ni njia ya kisasa inayowezesha mtu kulima bila kuwa na shamba kubwa. Hata ukiwa na eneo dogo, unaweza kupata mazao ya kutosha kwa matumizi ya familia na hata ziada ya kuuza” alieleza Kimweri.

Aliendelea kusema kuwa katika maonesho ya Nanenane kwenye kitalu cha halmashauri, mboga na matunda ya aina mbalimbali yamepandwa. “Katika kipindi hiki cha Nanenane tuko na baadhi ya mboga ambazo zimelimwa kwenye vichuguu vyetu ambazo ni brokoli, kabeji za kawaida, kabeji nyekundu, chainizi, spinachi na sukuma wiki. Mboga hizi hustawi vizuri kwenye mazingira ya mjini na huhitaji uangalizi wa wastani tu ili kutoa mavuno bora. Pia tuna bustani viroba, nyumba vitalu na bustani za nyumbani ili kujipatia mboga safi kwa matumizi ya kila siku. Kwa wale wanaoishi kwenye nyumba za kupanga au kwenye maeneo yenye nafasi ndogo sana, nyumba vitalu ni suluhisho bora. Hizi ni bustani zilizojengwa kwa muundo unaofanana na kibanda kidogo, zenye wavu maalum kuzuia kuku na wanyama wengine wasiingie. Uzuri wa nyumba kitalu ni kwamba unaweza kuibeba na kuhama nayo unapohama, jambo linalowapa uhuru wakazi wa mjini kuendelea na kilimo popote walipo” alisema Kimweri.

Kwa upande mwingine, Afisa Kilimo katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Emmanuel Mayyo alisema kuwa kilimo cha alizeti na mahindi ni miongoni mwa mazao ya kimkakati kwa wakulima wa Dodoma yenye kuchangia usalama wa upatikanaji wa chakula. Alizeti ikileta kipato kupitia uzalishaji wa mafuta kwa matumizi ya nyumbani na biashara.

Alisema kuwa zao la alizeti ni miongoni mwa mazao yenye tija kwa wakulima mkoani Dodoma. “Alizeti ni zao la biashara linalopendwa kwa sababu ya uwezo wake wa kuzalisha mafuta ya kula na ambayo yanauzwa ndani na nje ya mkoa. Biashara ya mafuta ya alizeti inawapatia wakulima kipato cha ziada na kuchochea maendeleo ya kiuchumi. Nawasihi wakulima kutumia teknolojia za kisasa ili kuimarisha usalama wa chakula na kuongeza kipato” alisema Mayyo.

MWISHO

Imehaririwa na Nancy Kivuyo

Comments

Popular Posts

Mfumo wa Ufuatiliaji na Tathmini ni nyenzo ya utendaji kazi serikalini – Dkt. Biteko

JIJI LA DODOMA KUPELEKA MIL 50 ZAHANATI YA KIKUYU

WENZA WA VIONGOZI WASHAURIWA KUANZISHA BUSTANI ZA NYUMBANI