Rais Samia: Tumieni kikamilifu Miundombinu, Teknolojia na mitaji iliyowekezwa katika Kilimo, Uvuvi na Mifugo

Na. Mwandishi wetu, DODOMA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amewataka wananchi, Wizara na Taasisi zinazohusika na sekta za kilimo, mifugo na uvuvi kutumia kikamilifu miundombinu, teknolojia na mitaji iliyowekezwa na Serikali ili kuongeza tija na ushindani wa Taifa katika masoko ya ndani na nje.



Akizungumza katika kilele cha Maonesho na Sherehe za wakulima, wafugaji na wavuvi (Nanenane) zilizofanyika kitaifa katika Viwanja vya Nzuguni, Rais Dkt. Samia amesema miradi ya umwagiliaji iliyokamilika na inayoendelea kutekelezwa inapaswa kusimamiwa kwa viwango bora ili kuongeza eneo la kilimo cha umwagiliaji na kukuza tija ya mavuno.

Alieleza kuwa Serikali ya Awamu ya Sita imeongeza bajeti ya kilimo ili kugharamia ujenzi na ukarabati wa skimu za umwagiliaji, mabwawa na visima, pamoja na kuanzisha mashamba makubwa ya pamoja, huku upatikanaji wa mbegu bora na mbolea ya kisasa ukiimarika kupitia ruzuku na kuanzishwa kwa viwanda vya uzalishaji, hatua iliyoongeza matumizi ya pembejeo nchini.

Aliongeza kuwa ongezeko hilo la bajeti limewezesha miradi ya kimkakati chini ya Mpango wa Maendeleo ya Sekta ya Kilimo Awamu ya Tatu (ASDP III), huku Serikali ikiimarisha huduma za zana za kilimo na kuendelea kutoa ruzuku ya mbolea, sambamba na kuhimiza elimu ya matumizi sahihi kwa wakulima.

Rais, Dkt. Samia pia aliagiza maafisa ugani nchini kote kuendelea kutoa elimu ya matumizi ya pembejeo na kuhakikisha zana za kilimo zilizopo zinatunzwa vema ili zitumike katika shughuli za uzalishaji.

Akizungumzia upatikanaji wa mitaji, Rais Dkt. Samia amesema Serikali imewezesha sekta ya kilimo kwa kutoa mikopo yenye masharti nafuu na kuanzisha Benki ya Ushirika. Tanzania yenye lengo la kusaidia wakulima, wafugaji na wavuvi kuwekeza kwenye miradi yenye mnyororo wa thamani.

Kuhusu Programu ya Jenga Kesho Iliyo Bora (BBT), Rais, Dkt. Samia alisema kuwa serikali imeendelea kutenga maeneo makubwa ya uzalishaji kwa vijana na wanawake yenye zana za kisasa pamoja na kuwapatia mikopo ya riba nafuu ya uendeshaji.

Kuhusu sekta ya mifugo, Rais, Dkt. Samia alieleza kuwa serikali imetenga ardhi kwa ajili ya malisho, imewezesha vijana kujiajiri kwenye ufugaji sambamba na kuzindua Kampeni ya Kitaifa ya Chanjo na Utambuzi wa Mifugo yenye lengo la kudhibiti magonjwa na kuongeza thamani ya mazao ya mifugo.

Kwa upande wa uvuvi, alisema kuwa serikali inaendelea kutoa mikopo ya boti, vizimba na vifaa vya kisasa pamoja na uwekezaji katika Bandari ya Uvuvi ya Kilwa itakayoongeza ajira na kuimarisha shughuli za uvuvi wa bahari kuu.

Katika hatua nyingine, Rais, Dkt. Samia alizindua Maabara Kuu ya Kilimo yenye viwango vya kimataifa, itakayokuwa kitovu cha maabara zote za kilimo nchini. Maabara hiyo inajumuisha maabara ndogondogo 15 zenye uwezo wa kufanya uchunguzi wa mimea, wadudu, udongo, sumu kuvu, afya ya mimea na kuzalisha miche isiyo na magonjwa pamoja na kuboresha ubora wa mbegu.

Rais, Dkt. Samia aliitaka maabara hiyo kujikita katika kazi za kisayansi na utafiti kwa umakini mkubwa, kwa kuzingatia kwamba jukumu hilo ndilo msingi wa usalama wa chakula wa Taifa, sambamba na kuagiza uanzishaji wa maabara maalum ya utafiti wa mbegu za asili, akisema hifadhi na utafiti wa mbegu hizo ni suala nyeti kwa mustakabali wa kilimo nchini.

Rais, alisisitiza kuwa sekta za kilimo, mifugo na uvuvi ni nguzo za mageuzi ya uchumi wa Taifa kwa mujibu wa Dira ya Maendeleo 2050 na Agenda 10/30 na kuahidi kuendelea kuwekeza, kuwasikiliza wadau na kutumia TEHAMA ili kuongeza ushindani katika sekta hizo.

Akirejea kaulimbiu ya maonesho ya Nanenane ya mwaka huu “Chagua Viongozi bora kwa Maendeleo Endelevu ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi 2025”, Rais, Dkt. Samia aliwahimiza wananchi kujitokeza kwa wingi siku ya tarehe 29 Oktoba ili kushiriki Uchaguzi Mkuu na kusisitiza kuwa kuchagua viongozi bora ni nguzo ya maendeleo ya Taifa.


Chanzo Blog ya Fullshangwe

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

RC Dodoma apongeza wafugaji kwa ushiriki wa Paredi ya Mifugo