IAA Tawi la Dodoma kuendelea kulea wataalam kwa vitendo

Na. Alex Sonna, DODOMA

CHUO cha Uhasibu Arusha (IAA) – Tawi la Dodoma, kimeendelea kuwa kinara katika kutoa elimu ya vitendo kwa vijana nchini, tangu kuanzishwa kwake mwaka 2021 kwa kuanza na programu tatu za diploma.


Akizungumza katika banda la Chuo hicho katika Maonesho ya Kitaifa ya Wakulima (NaneNane) yanayoendelea katika Uwanja wa Nzuguni, jijini Dodoma, Meneja wa tawi hilo, Dkt. Grace Temba, alisema kuwa chuo hicho ni sehemu ya mtandao wa kitaaluma unaojumuisha kampasi mama iliyopo Dar es Salaam, pamoja na matawi mengine yaliyopo Babati, Songea, Bukombe, Arusha, na Dodoma yenyewe.

“Tunapokea wanafunzi kuanzia ngazi ya kidato cha nne ambao husoma kwa miaka mitatu, wakijifunza kupitia mitalaa ya kisasa inayolenga kuwaandaa kwa soko la ajira la sasa na la baadaye,” alisema, Dkt. Temba.

Kwa sasa, IAA inatoa jumla ya programu 38 katika nyanja mbalimbali ikiwa ni pamoja na Uhasibu, Usimamizi wa Fedha, Uhasibu wa Kodi, Uongozi na Utawala wa Biashara, Masoko, na Usimamizi wa Ununuzi na Ugavi. Kozi hizi zimebuniwa kwa uangalifu ili kumwandaa mwanafunzi kuwa mtaalamu mahiri na mwenye ushindani katika mazingira ya kazi.

Dkt. Temba alieleza kuwa mafunzo ya diploma yanayotolewa chuoni hapo yanazingatia mfumo wa elimu shirikishi unaowapa wanafunzi nafasi ya kujifunza kwa vitendo, jambo linalowajengea uwezo wa kujitegemea na kuwa na ujasiri wanapoendelea na shahada au kuingia kwenye soko la ajira.

“Tunajivunia kuwalea vijana wanaoweza kushindana kitaifa na kimataifa kwa kuzingatia mabadiliko ya teknolojia na hali ya soko la ajira,” alieleza Dkt. Temba.

Alisema kuwa ushiriki wa IAA katika maonesho ya Nanenane ni wa kila mwaka, ambapo chuo hutumia fursa hiyo kutoa elimu kwa umma kuhusu kozi mbalimbali, taratibu za kujiunga, na nafasi zilizopo kwa vijana kujiendeleza kielimu.

Aidha, aliongeza kuwa kupitia banda la chuo hicho katika maonesho hayo, wananchi wamekuwa wakipata maelezo ya kina kuhusu huduma na fursa zinazopatikana, sambamba na ushauri wa kitaaluma. “Tunatumia jukwaa hili pia kuhamasisha vijana wa maeneo ya karibu na Dodoma kujiunga na kozi zenye tija, hasa zinazokidhi mahitaji ya sekta za fedha, biashara, utawala na TEHAMA,” alisema Dkt. Temba.

Kwa upande wa mikakati ya baadaye, chuo hicho kinaendelea kuimarisha mitaala yake, kuongeza matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano (TEHAMA) katika ufundishaji, pamoja na kujenga ushirikiano na wadau mbalimbali kwa lengo la kuongeza fursa za mafunzo ya vitendo kwa wanafunzi.

Alisema kuwa Chuo pia kinatumia fursa hiyo kuonyesha namna kinavyotekeleza mkakati wa Serikali wa kuimarisha elimu na taaluma kwa vitendo, jambo linalosaidia kuongeza ajira kwa vijana na kukuza uchumi wa taifa.

Dkt. Temba ametoa wito kwa wazazi, walezi na wanafunzi kutembelea banda la IAA katika maonesho ya Nanenane ili kupata taarifa muhimu na kujifunza namna ya kuchagua kozi zenye mwelekeo bora wa ajira.

 

 

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

RC Dodoma apongeza wafugaji kwa ushiriki wa Paredi ya Mifugo

Rais Samia: Tumieni kikamilifu Miundombinu, Teknolojia na mitaji iliyowekezwa katika Kilimo, Uvuvi na Mifugo