Mkoa wa Dodoma kuja na Mpango Mkakati wa kukuza na kutangaza Utalii wa Ndani

Na. Hellen Minja, DODOMA RS

Utalii unatajwa kuwa na athari chanya za kiuchumi kwa mtu mmoja mmoja na Mkoa kwa ujumla pale unapotumika kimkakati. Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule amebainisha hayo alipokua akifungua kikao Maalumu cha Maandalizi ya uzinduzi wa Kitabu cha Mpango Mkakati wa Kukuza na Kutangaza Utalii wa Mkoa huu.



Kikao hicho kimewahusisha wadau wa utalii kutoka sekta mbalimbali waliokutana kwenye ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma jijini hapa lengo likiwa ni kupitia Mpango Mkakati ulioandaliwa sambamba na kuunda Kamati itakayoshughulikia kwa karibu ufanikishaji wa shughuli hiyo.

“Utalii una athari nyingi za kiuchumi kama ukiwa nao maana utakuza uchumi wa mtu mmoja mmoja lakini pia wa Mkoa. Dodoma tunatamani tuwe ‘hub’ ya utalii kwa sababu tunafikika kila upande wa nchi ya Tanzania hata kama vivutio vya utalii havipo Dodoma tunataka iwe active kwenye suala la utalii” Senyamule.

Akizungumza katika kikao hicho, Katibu Tawala Msaidizi Sekta za Viwanda, Biashara na Uwekezaji  Mwajabu Nyamkomora, amesema uwekezaji uliofanywa na Serikali katika miundombinu, utasaidia kuhabarisha umma juu ya maeneo yenye fursa za uwekezaji kwenye Utalii ambapo Mpango Mkakati huo pia, utafungua sura kwa wanadodoma na Watanzania kutambua fursa zilizopo.

Kadhalika, Nyamkomora aliwapitisha Wajumbe kwenye maudhui yaliyomo ndani ya Kitabu hicho kilichoshiba taarifa za vivutio adhimu vya Utalii vinavyopatikana katika Halmashauri za Mkao wa Dodoma ambavyo vingi havijulikani kama vinapatikana Mkoani hapa.

Kitabu cha Mpango Mkakati wa kukuza na kutangaza Utalii Mkoa wa Dodoma kinatarajiwa kuufungua mkoa huu kwa vivutio vya Utalii ambapo Sekta hiyo ni moja ya vipaumbele vya Serikali ya Mkoa katika kuinua uchumi wa Wananchi na wa Mkoa kwa ujumla, kitabu hicho kinatarajiwa kuzinduliwa rasmi kwenye hafla itakayofanyika Agosti 04, 2025 katika Ukumbi wa Mabele jijini hapa.

 

 


Comments

Popular Posts

Dkt. Mpango ahimiza elimu kwa jamii juu ya utunzaji wa Mazingira

Shilingi Bilioni 7 zatekeleza miradi ya maendeleo Kata ya Miyuji