Baraza la Biashara kuvutia sekta binafsi kuwekeza Dodoma

Na. Nancy Kivuyo, MTUMBA

Mwenyekiti wa Baraza la Biashara la Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri ameeleza kuwa Jiji la Dodoma linakua kwa kasi kutokana na uwezeshaji mkubwa unaofanywa na serikali katika miundombinu mbalimbali.




Aliyasema hayo katika kikao cha Baraza la Biashara la Wilaya ya Dodoma kilichofanyika katika ukumbi mkubwa wa mikutano wa halmashauri katika Mji wa Mtumba.

Alisema kuwa anapongeza mwitikio wa sekta binafsi katika uwekezaji Dodoma. “Ninyi watu wa sekta binafsi nawapongeza sana kwa kufanya uwekezaji wenye tija ikiwemo hoteli kubwa za kisasa zipo hapa Dodoma, kumbi za mikutano na maduka makubwa” alisema Shekimweri ambae pia ni Mkuu wa Wilaya ya Dodoma.

Aliongeza kuwa analipongeza Baraza la Biashara la Wilaya kwa kuweka sera za kuvutia wawekezaji. “Nalipongeza baraza hili kwa kuweka sera Madhubuti zinazofanya wawekezaji kuzikimbilia fursa zilizopo ndani ya Jiji letu la Dodoma. Tuendelee kufanya vizuri kwasababu hapa ndipo kitovu cha makao makuu ya nchi kilipo” aliongeza Shekimweri.

Alimalizia kwa kuwataarifu baraza kuwa Halmashauri ya Jiji la Dodoma inatekeleza mradi wa ufungaji kamera za usalama katika barabara zote kuu kwa lengo la kuimarisha ulinzi na usalama wa jiji lote. Ndugu zangu, halmashauri inatekeleza mradi wa ufungaji camera za usalama katika jiji letu na unatarajiwa kukamilika Agosti 30, 2025. Lengo la kuweka kamera hizi ni kuimarisha ulinzi na usalama wa jiji letu, kwa mantiki hiyo tunatarajia vitendo viovu na uhalifu havitakuwepo kwasababu tutaona kila kinachofanyika katika barabara zetu” alimaliza Shekimweri.




Kwa upande mwingine, Katibu wa Baraza la Biashara la Wilaya ya Dodoma, Dkt. Frederick Sagamiko alitoa rai kwa sekta binafsi kuendelea kushirikiana na serikali. “Naendelea kuwapongeza sekta binafsi lakini pia natoa rai tuendelee kushirikiana na halmashauri kuhakikisha maeneo ya maegesho kwa wafanyabiashara yanapatikana ili kuweka mazingira rafiki na wezeshi ya ufanyaji biashara. Halmashauri imekwisha tenga maeneo ya kibiashara ikiwemo Nala, Njedengwa, Iyumbu, Ihumwa, Msalaton a Hombolo. Maeneo haya ni mazuri kwa uwekezaji tuchangamkie fursa hizi” alisema Dkt. Sagamiko ambae pia ni Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Baraza la Biashara la Wilaya hukaa vikao kila robo kwa lengo la kujadili na kutengeneza mazingira rafiki ya ufanyaji biashara na kuvutia uwekezaji katika Jiji la Dodoma.  

Comments

Popular Posts

Shilingi Bilioni 7 zatekeleza miradi ya maendeleo Kata ya Miyuji

Dkt. Mpango ahimiza elimu kwa jamii juu ya utunzaji wa Mazingira