Mexime awaonya mastaa Dodoma Jiji FC, aitaja nafasi ya tano

Na. Mussa Richard, DODOMA.

Kocha Mkuu wa Klabu ya Soka ya Dodoma Jiji FC, Mecky Mexime amewataka wachezaji wa timu hiyo kuzingatia yale waliyojifunza kwenye uwanja wa mazoezi ili kuhakikisha wanashinda mchezo dhidi ya Singida Black Stars na waweze kutimiza malengo waliyojiwekea kwa msimu huu.



Mexime aliyasema hayo wakati wa mkutano na waandishi wa habari kuelekea mchezo huo ambapo walima zabibu wa Dodoma Jiji FC watavaana na kikosi cha Singida Black Stars ikiwa ni duru ya lala salama ya Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara, mchezo unaotarajiwa kuvurumishwa majira ya saa 10 kamili jioni katika uwanja wa Jamhuri Dodoma.

“Tumejiandaa kuhakikisha tunafanya vizuri kwenye mchezo huu ili tuweze kusogea nafasi za juu zaidi kwasababu nafasi ya tano bado iko wazi kwa yeyote atakayechanga karata zake vizuri ataweza kuishika. Sisi Dodoma Jiji FC mipango yetu ni kufika nafasi ya tano, kikubwa ni wachezaji kuzingatia kile tulichojifunza kwenye uwanja wa mazoezi na kuja kukionesha uwanjani” alisema Mexime.

Nae, Nahodha wa Timu ya Dodoma Jiji FC, Augustino Nsata alielezea maandalizi ya timu kuelekea mchezo dhidi ya Singida Black Stars huku akiwaita mashabiki wa Dodoma Jiji FC na wapenzi wa soka kujitokeza kwa wingi uwanjani kuiunga mkono timu yao. “Kiujumla sisi wachezaji na benchi la ufundi tumejiandaa vizuri kwenda kuchukua alama zote tatu japo tunajua Singida wana mwalimu mzuri na wana kikosi kizuri. Hilo halitupi hofu kutokana na maandalizi tuliyofanya, kikubwa tunawaomba wapenzi, mashabiki na wapenda soka kiujumla wajitokeze kwa wingi kutuunga mkono ili tuweze kufanya vizuri na kubakiza alama tatu nyumbani” alisema Nsata.

Kwasasa Dodoma Jiji FC, inashika nafasi ya 7 kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara ikikusanya alama 34 kibindoni, ikishuka dimbani kwenye michezo 28 na kufunga mabao 27. Vinara wa upachikaji mabao kwa Timu ya Dodoma Jiji FC msimu huu ni Paul Peter mwenye mabao 8 na Idd Kipangwile mwenye mabao 6 huku klabu hiyo ikiwa na michezo miwili mkononi.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

RC Dodoma apongeza wafugaji kwa ushiriki wa Paredi ya Mifugo

Rais Samia: Tumieni kikamilifu Miundombinu, Teknolojia na mitaji iliyowekezwa katika Kilimo, Uvuvi na Mifugo