Dkt. Mpango ahimiza elimu kwa jamii juu ya utunzaji wa Mazingira

Na. Nancy kivuyo, DODOMA

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Philip Mpango atoa rai kwa tasnia ya habari, taasisi na wananchi wote kushirikiana kutoa elimu kwa jamii juu ya utunzaji wa mazingira ili kupunguza madhara yatokanayo na uharibifu wa mazingira.


Aliyasema hayo akiwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya Siku ya Mazingira Duniani kitaifa yaliyofanyika jijini Dodoma katika ukumbi wa Jakaya Kikwete.

Dkt. Mpango alisema kuwa suala la usimamizi wa mazingira ni la kipaumbele katika maendeleo ya nchi. “Waheshimiwa viongozi mliopo hapa, chanzo kikubwa cha uharibifu wa mazingira ni tabia ya watu na pia mabadiliko ya tabia nchi. Yote haya hasara yake kidunia ni makubwa sana, takriban dola bilioni 300-600 kila mwaka zinapotea. Kwa mantiki hiyo ili kupata mazingira safi lazima wote tuwajibike” alisema Dkt. Mpango.

Aliongeza kuwa nchi yetu inapambana kuhakikisha kwamba kwa miaka ijayo taka za pastiki zitokomezwe kwa kiwango kikubwa. Taka hizi za plastiki zinatelekezwa hasa baharini na kusababisha joto na uharibifu. “Ongezeko la taka ngumu na plastiki linaongezeka kwa kasi sana. Katika maadhimisho haya hapa nchini kwetu kaulimbiu inasema ‘Mazingira yetu na Tanzania ijayo, tuwajibike sasa kudhibiti matumizi ya plastiki’ lengo la kaulimbiu hii ni kuielimisha jamii ya kimataifa na wananchi kwa ujumla ili kulinda vyanzo vya maji na mazingira dhidi ya athari za taka za plastiki na kupunguza matumizi ya bidhaa za pastiki kupitia uzalishaji endelevu” aliongeza Dkt. Mpango.


Aliendelea kusema kuwa urejelezaji wa taka bado ni wa kiwango cha chini na menejimenti ya taka ngumu nayo imeelemewa katika utendaji kazi wao kutokana na changamoto walizonazo za upungufu wa miundombinu.

Aligusia kuwa miongozo na mikakati mbalimbali ya kuhakikisha utunzaji wa mazingira unafikia lengo inafanyika ili kuijenga Tanzania iliyo salama kwa vizazi vya baadae. “Waheshimiwa viongozi, baadhi ya miongozo iliyowekwa ni pamoja na kuweka katazo la mifuko na vifungashio vya plastiki, kushirikisha wadau mbalimbali ambapo makampuni nane yalikubali na kutengeneza umoja wao. Ipo mikakati kadhaa ilibuniwa kusaidia kupunguza uchafuzi wa mazingira ambayo ni wajibu wa wazalishaji, muongozo wa menejimenti ya taka ya mwaka 2019 na mkakati wa ‘re-use, reduce and reycle’. Kwa mujibu wa ripoti ya Umoja wa Mataifa ya mwaka 2023 inayosimamia mazingira inaeleza kuwa uchafuzi wa plastiki utaweza kupunguzwa kwa hadi asilimia 80 ifikapo mwaka 2040 endapo nchi na wadau wa mazingira zitaweka sera thabiti za kufanya mabadiliko katika upunguzaji wa taka katika masoko kwa kutumia teknolojia yenyewe” aligusia Dkt. Mpango.

Alimalizia kwa kutoa rai kwa taasisi zote na waandishi wa habari kujikita katika kutoa elimu kwa jamii ili kusaidia kupunguza uharibifu wa mazingira. “Natoa rai kwa wadau wa mazingira na taasisi mbalimbali kutoa elimu bila kuchoka ili tuokoe jamii yetu ya sasa na ya baadae. Nampongeza Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jitihada zake za kuhamasisha matumizi ya nishati safi ili kuoka mazingira yetu na niwaombe nyote mliopo hapa mkawe mabalozi wazuri ili tuokoe mazingira ya Afrika na Dunia kwa ujumla” alimaliza Dkt. Mpango.



Nae, Mkuu wa Seksheni ya Maliasili na Utalii Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Happiness Karugaba alisema kuwa siku ya Mazingira Duniani, Halmashauri ya Jiji la Dodoma ilianza kuadhimisha tangu tarehe 1 Juni kwa kupanda miti 150 katika maeneo mbalimbali ikiwemo shule. “Tunaendelea kuhamasisha wananchi kutunza mazingira kwa kupanda miti hasa katika shule mbalimbali za hapa jijini na zoezi hilo litaendelea kuwa endelevu” alisema Karugaba.

Katika hatua nyingine, Mkurugenzi wa In and Out Gardens Enterprise, Shemsa Rukubayunga alishukuru kwa uwepo wa maadhimisho hayo kwasababu yanaongeza elimu kwa jamii. “Sisi kampuni yetu tunatunza mazingira kupitia upandaji wa maua, ni jambo jema sana kutunza mazingira ili kuokoa ikolojia inayopotea kupitia uharibufu wa plastiki na taka nyingine ngumu” alisema Rukubayunga.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

RC Dodoma apongeza wafugaji kwa ushiriki wa Paredi ya Mifugo

Rais Samia: Tumieni kikamilifu Miundombinu, Teknolojia na mitaji iliyowekezwa katika Kilimo, Uvuvi na Mifugo