Watumishi Zahanati Kitelela mambo shwari


Na. Mussa Richard, DODOMA

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule ametembelea na kukagua nyumba ya watumishi wa Zahanati ya Kitelela iliyopo Kata ya Nzuguni, Wilaya ya Dodoma na kuwataka watumishi kutoa huduma bora kwa wananchi.



Nyumba hiyo ‘two in one’ imegharimu kiasi cha shilingi 60,000,000 hadi kukamilika kwake, ikiwa na uwezo wa kukaliwa na familia mbili kwa pamoja.

Baada ya kukagua nyumba hiyo alisema “utekelezaji wa mradi huu ni muendelezo wa utekelezaji wa maagizo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuhakikisha tunapunguza vifo vya mama na mtoto, hasa wakati wa kujifungua, dhamira ya mradi huu ni kuimarisha na kusogeza huduma za afya karibu na wananchi. Mwanzoni huduma za afya zilikuwa zikitolewa lakini ikifika jioni huduma zinakuwa hazitolewi kutokana na wauguzi kuishi mbali na kituo cha afya. Lakini kwasasa muda wowote wananchi wa Kitelela na maeneo jirani wana uwezo wa kupata huduma muda wowote baada ya mradi huu wa nyumba za wauguzi kukamilika”.

 


Nae, Alhaji Jabir Shekimweri, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma akatoa pongezi kwa wananchi wa Kitelela kwa kukamilika kwa mradi huo, ambao utakuwa mkombozi wa huduma ya afya kijijini hapo.

“Nitoe pongezi kwa wananchi wa Kitelela kwa kukamilika kwa mradi huu wa nyumba ya mtumishi, kwasababu ni mradi ambao mliuanzisha nyie wenyewe baada ya kuona kuna uhitaji. Kwahiyo, imani yangu ni kuwa mtaendelea kutumia huduma za afya za zahanati hii, moja ya changamoto ambazo bado zipo ni kukosekana kwa huduma ya maji, changamoto ambayo tayari imeanza kufanyiwa kazi kwa kuchimbwa kisima cha maji. Kisima ambacho kitasaidi kupatikana kwa maji ya kutosha katika zahanati” alisema Shekimweri.

“Mradi wa ujenzi wa Zahanati ya Kitelela umesaidia kupunguza changamoto za upatikanaji wa huduma za afya kwa wananchi hasa mama wajawazito ambao walikua wanatembea umbali mrefu kufuata huduma na sasa tumewasogezea huduma ya kliniki ya mama na mtoto na wananchi watapata huduma za afya muda wote” alisema Dkt. Sebastian Pima Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Mradi wa ujenzi wa Zahanati ya Kitelela ulianzishwa mwaka 2005, kituo kinapatikana Kata ya Nzuguni Mtaa wa Kitelela, ambapo hapo awali ilikua na majengo mawili ambayo ni jengo la OPD na jengo la ‘Maternity’ ambalo kabla ya mradi kukamilika lilikuwa likitumika kama nyumba ya mtumishi.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Mbunge Mavunde akabidhi Kompyuta kwa Kata 41 za Jiji la Dodoma

Wafanyabiashara wa Soko Kuu la Majengo Dodoma watarajia makubwa Mradi wa TACTIC

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma