Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Na. Halima Majidi, DODOMA

Wananchi wa Kata ya Makutupora, jijini Dodoma, wameeleza kilio chao juu ya changamoto kubwa zinazowakabili, zikiwemo ukosefu wa maji safi, matatizo ya umeme, pamoja na shule kuwa mbali, hali inayowakwamisha katika shughuli za kila siku.



Wakizungumza katika mkutano wa mkuu wa mkoa uliofanyika katika Kata ya Makutupora, baadhi ya wakazi wa eneo hilo wamesema wamekuwa wakikumbana na shida ya maji kwa muda mrefu, huku wakilazimika kutembea umbali mrefu kutafuta huduma hiyo muhimu.

Akitoa kero hiyo, mkazi wa Mtaa wa Sekondari, Pasisi James, alisema kuwa, tangu kuhamia katika mtaa huo ni miaka mingi hivyo ameiomba serikali kuwasogezea huduma ya maji kwa sababu imekuwa ni changamoto kubwa na hivyo kushindwa kuendelea na kazi zao za kila siku. “Maji ni tatizo hapa kwetu, tunamiaka mingi tangu kuhamia hapa, nimekuja hata kusoma sijui mpaka leo bado tunahangaikia maji, tunachukua maji kwa wachina dumu moja hilo hilo ufulie pamoja na kunywa, hapo naomba mtusaidie” alisema. 

Aidha, alieleza kuwa kwa upande wa shule wanawatoto wadogo wa miaka mitano na shule inayotegemewa ni Makutupora na Veyula, wanalazimika kutembea umbali mrefu. Hivyo, wanashindwa waandikisha watoto kutokana na shule kuwa mbali. “Umbali wa shule, watoto wengi wanashindwa kwenda shule kwa sababu hiyo. Hivyo, kungekuwa na uwezekano wa kupata gari kama wenzetu wanavyofanya na ikapatikana mia mbili, mia tatu ili watoto waweze kufika shuleni” alisema James.

Nae, Mkazi wa Makutupora, Victoria Madeje, alisema mbali na changamoto ya shule kuwa mbali na watoto kushindwa kwenda shule, pia alilalamikia uhaba wa huduma za umeme, wakidai kuwa baadhi ya maeneo bado hayajaunganishwa, hali inayosababisha usumbufu mkubwa kwa wakazi hao. “Nimejaza fomu mara mbili na sijawahi kupata umeme hata siku moja, hivyo tunashindwa kusaga hata chakula tunatoka kisae tunakuja kusaga Veyula tunashida, tunaomba angalau watuletee umeme watakao kuwa na uwezo watuletee mashine jamani hiyo ndio kero yetu mtaa wa 36, sekondari mpaka kisae” alisema Madeje.

Kwa upande wake Ndeliani Richard alimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa msaada wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) na kuomba huduma iwe endelevu kwa sababu inasaidia katika shughuli mbalimbali ikiwemo shamba na vifaa vya shule. “Tunaomba iwe endelevu, tunaambiwa mwezi wa tisa mkataba unaisha, lakini tunaomba mama asituchoke, tunaomba atusaidie bado wajukuu na watoto wengine wanasoma, tunafanya biashara ndogondogo tunamshukuru sana kwa msaada wake” alisema Richard.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Dkt. Frederick Sagamiko akijibu kero hizo alisema Halmashauri ya Jiji la Dodoma katika kuhakikisha inaunga mkono jitihada za kuwa kila mtoto anapata haki ya elimu, ilitenga kiasi cha shilingi milioni 50 kwaajili ya ujenzi wa shule ya msingi mama katika Kata ya Makutupora,  Mtaa wa Sekondari, ambapo mpaka sasa pesa hiyo haijatumika popote kutokana na zuio la eneo hilo, kwa sababu eneo lililotengwa kwaajili ya ujenzi wa shule hiyo ni la bonde. “Wananchi wanatakiwa kuwa na subira, bado eneo lipo katika zuio ni eneo la bonde nadhani kuna maelekezo yametolewa, ile kazi itakapokamilika Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, sisi tupo tayari wakati wowote kama tutaruhusiwa kuendelea pale tutajenga, tutakuja tuone ‘plan B’ kama tunafanje kama hilo eneo halitatumika” alisema Dkt. Sagamiko.

Sambamba na hayo, alielezea suala la kata hiyo kutengewa eneo kwaajili ya makaburi kwamba eneo lililopo limejaa na kuna maombi yaliofanywa na diwani wa kata kwa kuwasiliana na Magereza ambapo wameomba ekari 50, na mpaka sasa Magereza wanaendelea kuchakata taarifa hiyo kiofisi. “Wakikamilisha taratibu za kiofisi wataenda kutuonesha sisi Jiji tuje tupime tayari kwaajili ya kutumika kwa maziko” alisema Dkt. Sagamiko.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Rosemary Senyemula alikiri kuwepo kwa changamoto hizo na kusema kuwa juhudi zinaendelea kufanyika na ataendelea kuwasiliana na mamlaka husika ili kuhakikisha changamoto hizo zinapatiwa suluhisho la kudumu, pia amefafanua kuwa malengo ya Mkoa wa Dodoma ni kuhakikisha kila mwanadodoma anafurahia amani na utulivu na kuona kuwa kila mtu anainuka kiuchumi. “Ili uinuke kiuchumi ndugu zangu sio lazima uwe unapata fedha nyingi, wapo wanaopata milioni lakini hawana wanachokifanya inatka maarifa na hekima, hekima ya kupima nifanye hiki badala ya hiki, hivyo naomba hicho mnachokipata tuinuke kwenye uchumi” alisema Senyemule.

Sanjari na hayo aliwapongeza wananchi kwa kuona juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwapatia wananchi fedha za kujikimu. TASAF ameamua kufanya hivyo kwasababu huo ni utashi, aliongeza kuwa kwa wale wanaotaka miti ya maembe watapewa mti mmoja mmoja, amewataka kuitunza kwa sababu miti hiyo imenunuliwa kwa gharama. “Ameamua kuwa hawa ni wananchi wangu tuendelee kuwasaidia, ulizeni nchi nyingine kama wanatoa tu fedha bila ya mtu kufanya kazi yoyote, kwa kuangalia hali ya wananchi wake na kuwapatia fedha ya kujikimu” alihoji.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma