Senyamule awasisitiza wanufaika wa TASAF kutumia pesa kujiletea maendeleo

Na. Aisha Ibrahim, DODOMA

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, amewataka wanufaika wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) kutumia vizuri pesa wanayopewa na mfuko huo katika kufanyia shughuli mbalimbali za kuingiza kipato ili kujikwamua kiuchumi na kuondokana na dhana ya kuwa tegemezi katika jamii na taifa kwa ujumla.


Aliyasema hayo wakati akiwa kwenye ziara fupi ya kutembelea wanufaika wa Mfuko wa TASAF katika mtaa wa Mchemwa, Kata ya Makutupora, jijini Dodoma iliyokwenda na Kaulimbiu isemayo ‘TASAF, kwa pamoja tuondoe umaskini’.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, alisema kuwa miongoni mwa malengo ya TASAF ni kuhakikisha wanajamii wenye kipato cha chini wanainuka kiuchumi na kuwa na kipato cha juu ili kusaidia kuinua vipato vyao na familia zao kwa ujumla. “Mfuko wa TASAF umekuja ili kuwafanya wale wenye kipato cha chini kuongezeka na kuanza kupata kipato cha juu” alisema Senyamule.

Katika hatua nyingine, aliwahimiza wanufaika wa mfuko huo kuipa thamani pesa hiyo kwa kufanyia shughuli za maendeleo kwasababu malengo ya TASAF hayawezi kutimia ikiwa walengwa hawatakuwa na utayari wa kufanikisha dhamira hiyo. “Dhamira hii haiwezi kutimia ikiwa mlengwa hajataka kuitimiza kwasababu leo tunaweza kusema tugawe laki moja kwa kila mtu lakini yule mwenye dhamira tutakuta pesa hiyo imeongezeka na imekuwa laki mbili” alisema Senyamule.

Kwa upande wake, Mratibu wa TASAF ngazi ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Sekunda Kasese alifafanua kuwa katika Mtaa wa Mchemwa kuna kaya 25 zenye wanufaika wa mfuko huo ambao wanapokea pesa hizo kwa njia ya benki na wengine hupokea pesa taslimu.

Nae, mkazi wa Mtaa wa Mchemwa ambae ni mnufaika wa TASAF, Esther Chitojo, mwenye umri wa miaka 68, aliushukuru mfuko huo kwa kuwawezesha na kuwasaidia kuinua vipato vyao kwasababu wameweza kupiga hatua moja kwenda hatua nyingine kimaendeleo. “Nimeshukuru kuletwa kwa TASAF kwasababu imeweza kutuinua sana na maisha yetu yanaenda vizuri” alisema Chitojo.

Sambamba na hayo, alieleza kuwa kupitia pesa anazopata kutoka TASAF aliweza kununua mbuzi wawili walioweza kuzaliana na kufikia mbuzi 12 na baadae alibadirisha mbuzi hao na kupata ng'ombe jike wawili ambao hadi sasa wamezaliana na kufikia ng'ombe 12 wanaotoa maziwa ya kuuza na kumfanya aweze kujipatia Kipato.

Mbali zaidi, alisema kuwa aliweza kuanzisha kilimo cha zao la Choya ambapo baada ya mavuno hupeleka sokoni kuuza na kupitia fedha hizo alifanikiwa kujenga nyumba yenye vyumba vitatu na sebule moja. “Kupitia fedha ninazopata kutoka TASAF nilianzisha kilimo cha Choya na huwa ninauza pamoja na maziwa. Kwahiyo, kwa kuweka pesa kidogo kidogo nilianza kununua simenti, nikafyatua tofali lakini mwaka jana niliuza ng'ombe wawili nikanunua mbao na mabati na nilifanikiwa kujenga nyumba yenye vyumba vitatu na sebule” alisema Chitojo.

Malengo ya mfuko wa TASAF ni kuzinusuru kaya maskini zaidi kwa kuongeza vipato na fursa za kujikimu, kuboresha huduma za kiuchumi na kijamii, kuimarisha lishe bora, kuongeza mahudhurio ya watoto shuleni, na kuhakikisha upatikanaji wa huduma za afya.

MWISHO


Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma