Vilabu vya michezo vyashiriki mazoezi ya viungo vya mwili jijini Dodoma

Na. Aisha Ibrahim, Mailimbili-DODOMA

Vilabu mbalimbali vya michezo jijini Dodoma, vimejitokeza kwa wingi katika Bonanza la “Dodoma Aerobics Festival” msimu wa kwanza, lililofanyika katika kiwanja cha Chinangali Park, kuanzia saa 12:00 asubuhi mpaka saa 6:00 mchana kwa lengo la  kuwakutanisha wanamichezo wote kushiriki mazoezi mbalimbali ya kuimarisha viungo vya mwili.


Bonanza hilo liliandaliwa na kikundi cha wakufunzi wa michezo kutoka Jiji la Dodoma 'Dodoma Trainers Group' lilijumuisha mchezo wa kunyanyua uzito, kupasha mwili, kurukaruka na vikundi vya kukimbia.

Akizungumza wakati wa bonanza hilo, mgeni rasmi ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri, aliwasisitiza wana Dodoma kuendelea kufanya mazoezi kila siku hasa siku ya Jumamosi kama ambavyo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, alivyosisitiza kila mtanzania kujitengea siku ya kufanya mazoezi kwa lengo la kuimarisha viungo vya mwili. “Mazoezi ni afya, mazoezi ni tiba hivyo, nawapongeza sana waandaaji wa “Dodoma Aerobics Festival” kwa kuja na hiki kitu muhimu Jiji la Dodoma na kutambua umuhimu wa michezo” alisema Alhaj Shekimweri.

Aliongeza kuwa, ushiriki wa mazoezi mbalimbali huleta fursa ya watu kutoka maeneo tofauti kukutana na kujumuika kwa pamoja katika kuburudika na kubadilishana uwezo na uwelewa wa mambo mbalimbali yanayohusiana na michezo. "Mazoezi yana tafsiri nyingi na nikisema hivi najua wana mazoezi wananielewa kwasababu kijamii kujichanganya huleta fursa ya kukutana na marafiki na viongozi mbalimbali kuburudika nao na kubadilishana mawazo na uelewa wa masuala ya kimichezo” alisema Alhaj Shekimweri.

Kwa upande wake, Afisa Habari wa “Dodoma Aerobics Festival” Emmanuel Juma, alisema kuwa wanajivunia kuanzishwa kwa tamasha kubwa la kuwakutanisha wana mazoezi kutoka vilabu mbalimbali na kupata fursa ya kujumuika kwa pamoja kufanya mazoezi ya kuimarisha viungo vya mwili. “Hili ni tamasha ambalo limekusanya vilabu vyote vya 'jogging' na wafanya mazoezi kutoka vituo mbalimbali Jiji la Dodoma lakini pia wapo wengine wametoka Wilaya ya Bahi, Mkoa wa Morogoro, Mkoa wa Tabora na mikoa tofauti tofauti. Hivyo, nijivunie kuwa hili ni tamasha kubwa na la Kipekee hapa jijini Dodoma” alisema Juma.

Nae, mwalimu kutoka kituo cha kufanyia mazoezi “Home Fitness Center” kilichopo Kata ya Nzuguni, Ally Lwambo, alifafanua kuwa kila mtu ana wajibu wa kufanya mazoezi ya viungo vya mwili kila siku bila kuzingatia suala la unene au wembamba wa mwili ili kujenga ukakamavu na uwezo mzuri wa kufikiria. “Ni wajibu wa kila mtu kufanya mazoezi kwasababu mazoezi ni afya na hayana mwembamba wala mnene hivyo ukipata muda wowote wa kufanya mazoezi basi shiriki ipasavyo” alisema Lwambo.

Sambamba na hayo, mmoja kati ya washiriki wa mazoezi hayo Acxa Madinda, alishauri kuwa mazoezi hayo yasiishie kwa watu wazima badala yake hata watoto waandaliwe matamasha mbalimbali ya michezo ya kuimarisha viungo vya mwili kwasababu michezo ni kujifunza na kuburudika. “Kama mnavyoona mimi nilikuja na mtoto wangu na baada ya kufanya mazoezi amefurahi sana hivyo nìshauri haya matamasha yasiishie tu kwa watu wazima bali yaandaliwe hata kwa watoto ili nao waweze kuburudika” alisema Madinda.

Kufanya mazoezi ya mwili kuna faida nyingi muhimu kwa afya ya mtu kama vile husaidia kudhibiti uzito wa mwili, kusaidia kuondoa mafuta yasiyohitajika mwilini, kuimarisha misuli na mishipa husaidia kuboresha hali ya akili na kufikiri.

MWISHO.

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

Comments

Popular Posts

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma