Dodoma Jiji FC, Gari Limewaka

Na. Mussa Richard, DODOMA

Klabu ya Soka ya Dodoma Jiji FC, imeichakaza Klabu ya Soka ya Fountain Gate FC, kwa kuichapa bao Moja kwa nunge katika mchezo wa Ligi kuu ya NBC Tanzania bara, mchezo uliopigwa katika dimba la Jamhuri hapo jana, bao pekee la Dodoma Jiji FC, liliwekwa kimiani na mchezaji Idd Kipagwile, kwa mkwaju wa penati mnamo dakika ya 37 ya mchezo.




Baada ya mchezo kutamatika Kocha Mkuu wa Dodoma Jiji FC, Mecky Mexime alisema “niwapongeze wachezaji wangu kwa kupambana na kuhakikisha tunashida mchezo. Mchezo ulikua ni mgumu ukizingatia hatuna idadi ya wachezaji wengi wenye utimamu kimwili lakini wachezaji waliopo kwa uchache wao wameweza kuonesha umuhimu wao kwenye timu wamepambana kadri ya uwezo wao tumeweza kushinda mchezo, tumetengeneza nafasi kwa idadi kubwa sana kipindi cha pili lakini kutokana na presha ya mchezo tukashindwa kuzitumia lakini kwenye mchezo ujao tutajiandaa kwenda kuhakikisha tunatumia nafasi tunazotengeneza kwa usahihi”.


Akiongelea malengo ya timu alisema kuwa ni kukusanya alama kwa kila mchezo ulio mbele yao. “Ili kujiweka katika nafasi nzuri zaidi mwishoni mwa msimu, na ushindi huu mfululizo kwa mechi za nyumbani unatuongezea nguvu zaidi ya kupambana huku tukusubiri majeruhi wapone haraka warudi kwenye timu ili tuje tupambanie malengo yetu kwa pamoja” aliongeza Mexime.




Nae, nyota wa mchezo huo Mwanakibuta David baada ya dakika 90 kutamatika aliwashukuru wachezaji wenzake kwa kupambana kuhakikisha timu inapata matokeo chanya licha ya kukumbwa na wimbi la majeraha kwa baadhi ya nyota wake wa kikosi cha kwanza.


“Namshukuru Mwenyezi Mungu mchezo umeisha salama na tumeweza kupata alama tatu muhimu, lakini kwa ukubwa niwapongeze wachezaji wenzangu kwa kupambana kwa dakika zote mpaka tumefanikiwa kushinda mchezo wa pili mfululizo. Nitakuwa mchoyo wa fadhila nisipo washukuru mashabiki wetu ambao wamejitokeza kwa wingi kutuunga mkono, kama wachezaji tumefarijika sana na tutaendelea kujituma kuhakikisha mashabiki wanafurahi na timu inazidi kukusanya alama na kupanda katika nafasi za juu zaidi kwenye msimamo wa ligi” alisema Kibuta.



Katika michezo mitatu ya mwisho Dodoma Jiji FC, imefanikiwa kukusanya alama saba kibindoni, ikitoa sale mchezo mmoja, ikishinda michezo miwili. Mchezo ujao Dodoma Jiji FC, itasafiri kuwafuata Nyuki wa Tabora, Tabora United mchezo unaotarajiwa kuchezwa katika dimba la Ali Hassan Mwinyi Februari 28 saa 10:00 jioni.

Comments

Popular Posts

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma