Wafanyabiashara kuboresha huduma na kukuza biashara Mwaka 2025

Na. Halima Majid na Shahanazi Subeti, DODOMA

Wafanyabiashara waweka wazi malengo ya kuboresha huduma ya kukuza biashara zao na kuchangia maendeleo ya uchumi ya Jiji la Dodoma mwaka 2025.


Hayo yalisemwa na wafanyabiashara wa eneo la One Way lililopo katikati ya Jiji la Dodoma wakati wa mahojiano na waandishi wa habari walipokuwa wanaelezea salamu za jinsi walivyoupokea mwaka mpya 2025.

Mfanyabiashara wa urembo, Luqman Olomi, katika Mtaa wa One Way alisema changamoto kubwa ni matatizo ya kifamilia yanayopelekea kurudishwa nyuma kiuchumi na kusababisha biashara yake kuyumba kwa kiasi flani. "Kuna changamoto za kifamilia zaidi ambazo huwa zinaturudisha nyuma kwa kiasi kikubwa kwa sababu inabidi utumie mpaka kiasi ambacho umeweka kwa ajili ya biashara na ili tufanikiwe inatakiwa tujitegemee na tusitegemee cha mtu. Hiyo ndio siri ya mafanikio na kwa anayoyafanya Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kushirikiana na mashirika mengi na taasisi mbalimbali anafanya vizuri” alisema Olomi.

Nae Mfanyabiashara wa vitambaa, Barke Boda, alisema kuwa ana malengo ya kutafuta riziki yake na malengo makubwa ni kuendelea kutoka sehemu aliyopo kwasasa na kuikuza. “Mwaka huu nina malengo makubwa naomba Mungu anisimamie katika hilo. Kwa maana mwaka uliopita haukuwa mzuri kibiashara lakini tunamshukuru sana tunaendelea vizuri tunatakiwa tusikate tamaa tujipange vizuri ili tuweze kufikia malengo” alisema Boda.

Mfanyabiashara wa viatu na mabegi, Mwanahamisi Hamadi, alisema mwaka ameupokea vizuri na anamalengo ya kuendeleza biashara kwa kuongeza bidhaa zaidi na amesisitiza kuwa makini katika biashara ili kuepuka matapeli. “Licha ya changamoto nilizozipitia lakini pia nimesema kuwa nina malengo makubwa   mwaka huu kwasababu naamini utakuwa ni mwaka wa utulivu na ulinzi wa kutosha ili niweze kufanya biashara zangu kwa amani licha ya kuwa ni mwaka wa uchaguzi” alisema Hamadi.

 Mwaka 2025 unatarajiwa kuwa kipindi cha mageuzi makubwa kwa wafanyabiashara wa One Way huku wakiwa na matumaini ya kuimarisha uchumi wa familia zao na Jiji la Dodoma kwa ujumla.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma