Kambi: Watoto wenye mahitaji maalum wanahaki ya kusoma

Na. Coletha Charles, CHANG’OMBE

Kata ya Chang’ombe, Halmashauri ya Jiji la Dodoma imebainisha na kuwaandikisha watoto wenye mahitaji maalum kwa lengo la kujiunga na elimu ya awali na msingi kwa mwaka wa masomo 2025 kwa kushirikiana na wazazi, walezi na walimu.

 

Afisa Elimu Maalum Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Mwl. Issa Kambi akifanya uchunguzi mwanafunzi mwenye mahitaji maalum

Akizungumza wakati wa uandikishaji wa watoto hao, Afisa Elimu Maalum Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Mwl. Issa Kambi, alisisitiza kuwa jukumu la kuwapatia watoto hao fursa ya kusoma lipo mikononi mwa wazazi na walezi kwa sababu wanahaki ya kupata elimu kama watoto wengine kwa kuwajengea msingi bora wa maendeleo.

 

Alisema kuwa, serikali imejipanga kuwahudumia watoto wenye mahitaji maluum kwa kuwapokea na kuwapa mahitaji stahiki na kuhakikisha wanapata nafasi bila kujali changamoto zao. “Wazazi ukiwa na mtoto usichoke kumlea, ukiona umechoka basi huyo mtoto amefanikiwa na tusiwakatie tamaa. Watoto wenye umri wa kwenda shule tushirikiane kuwaleta waje waandikishwe kwenye shule zetu, walimu wapo watawahudumia. Niwaombe muwaambie na wengine waliobaki nyumbani kuwa, tunapokea watoto wa aina zote kulingana na mahitaji yao na tunawahudumia” alisisitiza Mwl. Kambi.

 

Nae, Afisa Elimu, Kata ya Chang’ombe, Rebecca Haule, alitoa wito kwa wazazi na walezi kuhakikisha watoto wenye mahitaji maalum wanapata fursa ya kuandikishwa shule kwa ajili ya kuanza masomo ili waweze kujifunza na kufikia ndoto zao.

 

Afisa Elimu Maalum Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Mwl. Issa Kambi alifafanua jambo

Alisema kuwa, kila mzazi mwenye mtoto ambaye ana umri wa kuanza kusoma anapaswa kumuandikisha ili aanze masomo kwa sababu elimu ni haki yake ya msingi na serikali ya awamu ya sita imeweka mazingira bora na rafiki ya kujifunza. “Kama kata tumejitahidi kuhamasisha na wazazi wamejitokeza, tutaendelea kuhamasisha hadi siku ya mwisho na tunawaomba wazazi na walezi watupe ushirikiano. Tunawaomba wasiache kuwapeleka watoto wenye mahitaji maalum shule, kwa sababu elimu ni msingi wa maendeleo ya mtoto na jamii kwa ujumla” alisema Haule.

 

Kwa upande wake, Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Chang’ombe, Mwl. Bakari Mtembo, alitoa wito kwa wazazi kutowafungia ndani watoto wenye mahitaji maalum na badala yake kuwapeleka shule kwa sababu wana haki ya kupata elimu kama watoto wengine.

 

Alisema kuwa, ubainishaji wa watoto wenye mahitaji maalum ni hatua muhimu katika kuhakikisha elimu jumuishi inatekelezwa kikamilifu na ushirikiano unahitajika ili kuhakikisha watoto hao wanapata msaada wanaohitaji kufikia ndoto zao. “Mwitikio wa wazazi kuwaleta watoto kuandikishwa kwa ajili ya masomo 2025 umekuwa mkubwa, japo wamefika kwa kuchelewa huenda hawakupata taarifa ya uandikishaji mapema kutoka kwa viongozi wao wa mitaa. Lakini pia shule yetu inapokea watoto wenye mahitaji maalum. Hivyo, wazazi wasione aibu kuwaleta watoto shule” alisema Mwl. Mtembo.

 


Aidha, mkazi wa Chang’ombe ambaye ni mzazi wa mtoto mwenye mahitaji maalum, Erika Magomba, aliomba serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwasaidia wazazi wenye watoto wenye mahitaji maalum misaada mbalimbali ya mahitaji katika ukuaji wao. “Niwashauri wazazi wenzangu kutowaficha watoto kwa sababu hawa watoto wengine wanavipaji mbalimbali kama kushona na ufundi. Kwahiyo, tujitahidi tuwatoe watoto nje ili watu wawaone waweze kuwasaidia. Ninawashukuru sana watoto wetu wamepata msaada mkubwa wa kwenda shule” alisema Magombe.

Katika harakati za kuhakikisha watoto wenye mahitaji maalum wanapata haki zao za msingi ya kupata elimu, umuhimu wa kubainisha changamoto zao mapema hauwezi kupuuzwa.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma