Miaka 63 ya Uhuru, watanzania waaswa kutunza na kuthamini Uhuru

Na. Faraja Mbise, DODOMA

Watanzania wameaswa kutunza na kuthamini uhuru kwa kufanya mambo yanayoleta amani na usalama wa nchi, ili kufurahia matunda ya uhuru yaliyopatikana ndani ya miaka 63 tangu tarehe 09 Desemba, 1961.




Hayo, yalisemwa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, alipokuwa akizungumza na mamia ya wananchi waliohudhuria katika kilele cha Maadhimisho ya Miaka 63 ya Uhuru wa Tanzania Bara yaliyofanyika katika makutano ya Barabara ya Mzunguko (Ring Road) katika Kata ya Makutupora, jijini Dodoma.

Senyamule alisema “ili uhuru huu tuendelee kuufurahia na kuuenzi, kwanza tuhimize amani na usalama wa nchi yetu kwasababu ni msingi wa mafanikio. Huu uhuru tunausherekea kwasababu bado tunaulinda, usije ukafikiri ukipata uhuru ndio imeisha, unaweza ukapata uhuru na baadae ukapotea tena kwasababu unaweza ukaingiliwa. Tuendelee kutunza kwa kufanya mambo ya amani na utulivu”

Akizungumzia mafanikio yaliyopatikana katika Miaka 63 ya Uhuru, aligusia mafanikio mbalimbali katika miundombinu na fursa zilizopo nchini ukilinganisha na miaka ya nyuma ambayo Tanzania Bara ilikuwa haijajipatia uhuru wake. “Ndugu zangu tunapoongelea Miaka 63 ya Uhuru, Mkoa wetu wa Dodoma unaendelea kukua kwa ‘speed ya 5G’ yaani kasi ya kukua kwa Mji wa Dodoma kila mtu anaishangaa, kuanzia sekta moja kwenda sekta nyingine. Leo tumesimama kwenye hiyo Barabara ya Mzunguko, barabara hiyo ya mzunguko haipatikani sehemu nyingine yoyote Tanzania, Afrika Mashariki, Afrika ya Kati, kwa ukubwa wake, upana wake na urefu wake, inapatikana Dodoma peke yake” alisema Senyamule.




Akiongelea kuhusu kaulimbiu ya maadhimisho ya Miaka 63 ya Uhuru wa Tanzania Bara, isemayo “Uongozi Madhubuti na Ushirikishwaji wa Wananchi ni Msingi wa Maendeleo yetu” alisema Tanzania inabahati kuwa na uongozi madhubuti ambao unafanya kila jitihada za kimaendeleo sambamba na kushirikisha wananchi katika kila hatua ya maendeleo ya nchi. “Sisi kama watanzania tunayo bahati kwasababu tumekuwa na uongozi madhubuti toka uhuru wa nchi yetu, watu wakianza kumuelezea Baba wa Taifa hawamalizi kurasa kwa sifa za uongozi wake. Vilevile, tumepata viongozi wazuri kwa kila awamu. Lakini kaulimbiu hii inaendelea kusema ushirikishwaji wa wananchi ni msingi wa maendeleo. Katika historia ya nchi yetu tumeshuhudia mambo mengi lakini kwa wakati huu ninaona ushirikishwaji umepita nyakati nyingine nyingi. Tunaona jinsi ambavyo Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan anavyotamani mambo yote yanayoamuliwa kwa ajili ya watanzania yatokane na watanzania wenyewe, ndio maana wakati wote utasikia anasema ninaunda tume, iende kwa wananchi ikapokee mawazo ili tuje tutengeneze jambo, kwasababu yeye anaamini katika ushirikishwaji” alisema Senyamule.

Kwa upande wake Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma, Prof. Davis Mwamfupe, aliwaasa wananchi katika kuadhimisha miaka 63 ya Uhuru wa Tanzania Bara, kuwajibika kwa kufanya kazi ili kuwa huru. “Hatuwezi kujidai tuko huru kama hatufanyi kazi, kwasababu bila kufanya kazi tutakuwa watumwa, kama sio mtumwa wa jirani, nchi jirani au nchi nyingine. Kwahiyo, msisitizo wangu mkuu katika hafla hii, uhuru ni kazi, usipofanya kazi hatutakuwa huru. Uhuru kama taifa unaanzia pale ambapo mtu mmoja mmoja anapokuwa na uhuru. Kwahiyo, tufanye kazi kama mtu binafsi, lakini tufanye kazi ili taifa letu liwe huru” alisisitiza Prof. Mwamfupe.

Vilevile, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Misitu Tanzania (TFS), Prof. Don Santos Silayo, aliwataka wananchi kuadhimisha miaka 63 ya Uhuru wa Tanzania bara kwa kushiriki katika kupanda miti ili kutunza ikolojia. “Siku ya leo tunapoadhimisha miaka 63 ya Uhuru wa Tanzania Bara, nchi yetu inaowajibu wa kulinda na kudumisha mazingira yetu kwasababu mazingira yetu ndiyo yanayotutunza sisi. Sisi hatuwezi kuwa salama kama mazingira sio salama. Kwahiyo, tunaowajibu wa kutunza, kwa dhamana ya leo na jambo tulilolifanya la kupanda miti ni jambo la kushukuru kwamba kila mmoja anapata nafasi ya kuona umuhimu wa kushiriki kwenye uumbaji” alisema Prof. Silayo.

Maadhimisho ya Miaka 63 ya Uhuru wa Tanzania Bara, jijini Dodoma yalianza na zoezi la upandaji miti katika eneo la barabara ya pete "ring road" katika eneo la Barabara ya Nala- Makutupora. Takribani miti 100,000 itapandwa kuzunguka eneo hilo, ambapo mashimo mia nane yamechimbwa na miti 800 ilitandwa, awali ilipandwa miti 850. Miti hiyo imepandwa kwa lengo la kuifanya Dodoma kuwa ya kijani ili kukabiliana na mabadiliko ya tabia ya nchi yanayoikumba Dunia kwa sasa.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma