Madiwani wadaiwa uthubutu kufanya maamuzi ya kimaendeleo

Na. Faraja Mbise, DODOMA

Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Kyerwa, mkoani Kagera, wametakiwa kuwa na uthubutu katika kufanya maamuzi ya kimaendeleo ili kuwanufaisha wananchi wanaowasimamia. Hayo yalisemwa na Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma, Prof. Davis Mwamfupe, alipokuwa akiwakaribisha madiwani kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Kyerwa, mkoani Kagera, katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma.


Mstahiki Meya, Prof. Davis Mwamfupe akifafanua jambo


“Kikubwa katika mtakachokiona, sio utajiri wetu wa pesa ni uthubutu wa kufanya maamuzi, unaweza kuwa na pesa lakini hauna uthubutu wa kuzitumia, ukipewa shilingi milioni moja, utapata wasiwasi kuzitumia kwasababu zitaisha, hutakubali matumizi ya laki mbili au tatu. Lakini sisi hatuogopi, kama tuna mradi wa hoteli iliyopo hapa ambayo imegharimu shilingi Bilioni 12, hatuogopi mradi wa Soko la wazi la Machinga, ingawa serikali ilituchangia shilingi Bilioni tatu, na sisi tukaweka shilingi bilioni sita nyingine. Hatuogopi kwamba tuliwekeza katika mradi na hoteli na ukumbi kule Mtumba, ambao kwa awamu mbili tulipanga uwe na shilingi bilioni 54. Karibuni Dodoma muweze kuangalia matokeo ya uthubutu wetu wa kufanya maamuzi. Sisi hatupendi kujadiliwa kwanini hatukuamua tunapenda tushtakiwe kwanini mliamua vibaya” alisema Prof. Mwamfupe.

Akizungumzia suala la maendeleo, aliwataka waheshimiwa madiwani kuunga mkono juhudi za Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika kukuza uchumi wa nchi na kutoa rai kuwa, wananchi wahudumiwe vizuri bila kutengeneza kero. “Tuungane na Mheshimiwa Rais, kuhakikisha kwamba, tunafikisha maendeleo bila kero yoyote kwa wananchi wanaotegemea huduma yetu” alisisitiza Prof. Mwamfupe.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Wilaya ya Kyerwa, SACF. James John, aliwataka madiwani hao kujifunza namna mbalimbali za kukusanya mapato kupitia ziara hiyo waliyoifanya ili kukuza uchumi wa Kyerwa. “Kwanini nilitamani tuje Dodoma, ni kwamba, kuamua ni bora sana kuliko kusitasita, lakini kuamua kwa manufaa ya taasisi, kwamba leo sisi tunafanya haya maamuzi makubwa watu hawatatuelewa, watatulaumu lakini kokote tutakakokuwa miaka ya mbeleni tutasema wakati sisi tuko kwenye halmashauri tulifanya moja na mbili. Kwahiyo, jambo ambalo natamani tuondoke nalo hapa ni kuthubutu kufanya bila kujali ‘size’ ya kipato chetu” alisema SACF. John.

Vilevile, Diwani wa Kata ya Matunguru, Halmashauri ya Wilaya ya Kyerwa, Florence Frederick, aliipongeza Halmashauri ya Jiji la Dodoma, kwa kuonesha uthubutu katika kuanzisha na kuendeleza miradi. “Nimejifunza mambo mengi katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, kupitia ziara hii, mfano Shule ya Dodoma English Medium School. Kwahiyo, tumejifunza na sisi tutaenda kufanya juhudi zetu tuwe na shule nzuri kama hiyo. Naipongeza Halmashauri ya Jiji la Dodoma, kwa mipango yake mizuri na mapato wanayopata, inaonekana walithubutu na sisi tutathubutu ili mambo yaende vizuri” alipongeza Frederick.




Madiwani hao waliwasili Halmashauri ya Jiji la Dodoma tarehe 17 Desemba, 2024 kwa ajili ya ziara ya siku moja, yenye lengo la kutembelea miradi ya kimkakati iliyopo jijini Dodoma na kujifunza uthubutu wa kufanya mambo mbalimbali ya kimaendeleo ili kuongeza mapato ya halmashauri yao.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma