Uchaguzi wa Serikali za Mitaa Wafanyabiashara wamo

Na. Faraja Mbise, DODOMA

Wafanyabiashara Halmashauri ya Jiji la Dodoma wamehamasishwa kujitokeza kushiriki katika mchakato wa Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa kujiandikisha kwenye orodha ya wapiga kura ili kupata viongozi walio bora ambao wanatambua wajibu wao ili kuwawezesha wafanyabiashara kutatua changamoto zao katika biashara.


Meneja wa Hoteli ya Spring Hills, William Mndeme akielezea umuhimu wa wafanyabiashara kushiriki Uchaguzi wa Serikali za Mitaa


Rai hiyo ilitolewa na Meneja wa Hoteli ya Spring Hills, William Mndeme alipokuwa akiongea na waandishi wa habari kuhusu umuhimu wa wafanyabiashara kujiandikisha katika orodha ya wapiga kura kwa ajili ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa.

Meneja Mndeme aliwashauri wafanyabiashara wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma kuitikia wito wa kwenda kujiandikisha ili waweze kuchagua viongozi walio bora na wenye manufaa katika kukuza uchumi wa nchi. “Ili tuweze kufanya biashara vizuri, lazima tuwe na viongozi bora na viongozi wanaotambua wajibu wao, ili kuweza kutusaidia sisi wafanyabiashara pale tunapokuwa na changamoto. Hivyo, ili kupata viongozi walio bora watakaowezesha mazingira ya biashara kuwa mazuri wafanyabiashara wanawajibu wa kujiandikisha kwenye orodha ya wapiga kura ili washiriki katika uchaguzi wa viongozi wa serikali za mitaa” alisema Mndeme.

Aidha, aliipongeza Kamati ya Usimamizi wa Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa hamasa ambazo zinaendelea huko mitaani kwa lengo la kuhamasisha wananchi kujitokeza kujiandikisha katika orodha ya wapiga kura katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa unaotarajiwa kufanyika tarehe 27 Novemba, 2024. “Zoezi la kujiandikisha linakwenda vizuri, lakini pia kila ninapopita ninaona mabango au kukutana na matangazo ya uchaguzi wa serikali za mitaa. Kwahiyo, linakwenda vizuri sijaona changamoto yeyote, ni zoezi ninaloona limeanza vizuri na linaenda vizuri, watu wanajiandikisha” alisema Mndeme.




Pia, alitoa rai kwa wafanyabiashara na wananchi wote kujitokeza kujiandikisha katika orodha ya wapiga kura kabla zoezi halifungwa. “Ninawaomba wafanyabiashara wenzangu waitikie hili kwa moyo wao mmoja kwasababu itakuwa ni faida kwetu, ningewaomba mpaka hiyo tarehe 20 wawe tayari wamejiandikisha ili tuweze kuchagua viongozi watakaotusikiliza maoni yetu. Pia ni haki ya kila mtanzania kujiandikisha, mtu aliyefikisha umri wa kupiga kura, mika 18 na kuendelea na uwe mkazi wa eneo husika, uwe raia wa Tanzania na uwe na akili timamu. Na mtu atakae jiandikisha katika eneo zaidi ya moja atakuwa amepoteza sifa za kuwa mpiga kura” alisema Mndeme.

Zoezi la kuandikisha wapiga kura katika orodha ya wapiga kura lilianza tarehe 11 Oktoba, 2024 na litaendelea hadi tarehe 20 Oktoba, 2024 na tarehe ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa ni 27 Novemba, 2024.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma