Sekunde chache kujiandikisha orodha ya wapiga kura

Na. Faraja Mbise, DODOMA

Urahisi wa zoezi la kujiandikisha katika orodha ya wapiga kura umekuwa kivutio kikubwa sana kwa wananchi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, kujitokeza na kushiriki katika uchaguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika ifikapo tarehe 27 Novemba, 2024.

Wakazi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma waliojitokeza kushiriki zoezi hilo la uandikishaji wameeleza urahisi wake kuwa halichukui muda mrefu.

Kwa upande wake Mariamu Paul, mkazi wa Mtaa wa Azimio, Kata ya Mpunguzi aliwashauri wananchi kujitokeza na kujiandikisha katika orodha ya wapiga kura kwasababu zoezi halichukui muda mrefu. Aliongeza kuwa ni haki yao ya msingi na inawapa fursa kubwa ya kuchagua viongozi wa serikali ya mtaa wanaowataka na kuwaasa wasisubiri kuchaguliwa na watu wengine. “Nimekuja kujiandikisha na nawashauri wananchi wengine waje. Nimetumia kama sekunde kadaa tu kwa sababu hata haizidi dakika moja kuandikishwa na haichukui hata muda wako” alisisitiza Paul.

Peter Agustino, mkazi wa Mtaa wa Kigamboni


Nae, Peter Agustino, mkazi wa Mtaa wa Kigamboni, Kata ya Kikuyu Kaskazini alimpongeza afisa muandikishaji katika Kituo cha Ofisi yaAfisa Mtendaji Kata ya Kikuyu Kaskazini kwa mapokezi mazuri, huduma nzuri wanayoitoa na lugha nzuri wanayotumia kupokea wananchi wanaoenda kuandikishwa. “Mapokezi ni mazuri, wanawakaribisha watu kwa lugha nzuri. Kiukweli nimefurahia kuhudumiwa hapa, mwandikishaji ni mkarimu mno” alisema Agustino.

Katika hatua nyingine Sylivester Bilingi, mkazi wa Mtaa wa Muungano, Kata ya Mkonze aliunga mkono juhudi za serikali katika kuhakikisha kuwa kila  mwananchi aliyekidhi vigezo vya kushiriki katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa anapata haki yake ya kuchagua au kuchaguliwa. Alisema, yeye kama mwananchi ataunga jitihada hizo kwa kutoa muda wake na kwenda kuwahamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki zoezi za kujindikisha katika orodha ya mpiga kura. “Nitaongea na mwananchi mmoja mmoja kumpatia elimu hii niliyoipata ya kujiandikisha katika orodha ya mpiga kura kwa ajili ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, ili na wenyewe wapate kuelewa umuhimu wa zoezi hili kabla muda wa kujiandikisha haujafika ukomo” alisema Bilingi.

Uchaguzi wa Serikali za Mitaa unatarajiwa kufanyika tarehe 27 Novemba, 2024 utakaotoa fursa kwa mwananchi kuchagua mwenyekiti wake wa kijiji, mwenyekiti wa vitongoji vilivyomo katika eneo la kijiji, wajumbe mchanganyiko wanawake na wanaume pamoja na wajumbe wa kundi la wanawake ambao idadi yao haitakuwa chini ya theluthi moja ya wajumbe wote wa halmashauri ya kijiji.

MWISHO

 

 

Comments

Popular Posts

Jiji la Dodoma lapewa angalizo lishe bora kwa wananchi

RC Dodoma apongeza wafugaji kwa ushiriki wa Paredi ya Mifugo

Rais Samia: Tumieni kikamilifu Miundombinu, Teknolojia na mitaji iliyowekezwa katika Kilimo, Uvuvi na Mifugo