KADI YA MPIGA KURA SIO LAZIMA KWENYE UCHAGUZI WA SERIKALI ZA MITAA

Na. Faraja Mbise, DODOMA

Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri, amewataka wananchi kujitokeza kwa wingi katika zoezi la kujiandikisha kwenye orodha ya mpiga kura zoezi litakalofanyika kwa muda wa siku kumi kuanzia tarehe 11- 20 Oktoba, 2024 na kusema kuwa kadi ya mpiga kura siyo kigezo cha kupigia kura.




Mkuu wa Wilaya ya Dodoma alisema hayo alipokuwa akizungumza na mamia ya watumishi wa umma na wananchi waliojitokeza katika Bonanza la kuhamasisha umma kujitokeza katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa katika Shule ya Sekondari Dodoma iliyopo Mtaa wa National Housing, Kata ya Makole jijini Dodoma.

Alhaj Shekimweri alisema “hakuna kadi ya mpiga kura kwenye Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, siku ya kupiga kura unaweza kwenda na kitambulisho chochote kile kama leseni ya udereva, kadi ya mpiga kura ya uchaguzi mkuu, kadi ya bima ilimradi utambulishwe na kadi yoyote. Na kama hauna kabisa basi hata jirani yako anaeaminika kuwa ni mkazi na ana kadi husika anaweza kukutambulisha”.

Aidha, aliwataka wananchi wazingatie muda wa kujiandikisha uliowekwa ili kusiwepo na malalamiko yoyote kwasababu muda wa kuorodhesha majina katika orodha ya mpiga kura hautaongezwa. pia alisisitiza Uchaguzi wa serikali ngazi ya mitaa ni mchakato wa kidemokrasia.




“Tunategemea uandikishwaji utafanyika kwa haraka na kwa kasi. Kwahiyo, muda uliowekwa wa uandikishaji unaonekana ni mrefu tukijipanga vizuri. Ndio tukaanza na bonanza hili ili tupeane elimu tukianza na watendaji pamoja na wenyeviti wa mitaa, tunataka mtumie nguvu nyingi kadri inavyowezekana mwanzoni ili mwishoni iwe ni kumalizia” alisema Alhaj Shekimweri.

Akiongelea tofauti kati ya zoezi uboreshaji daftari la kudumu la wapiga kura na uchaguzi wa serikali za mitaa alifafanua utofauti wake. “Uboreshaji wa daftari la kudumu la mpiga kura ulihitaji mtu ambae alishashiriki uchaguzi uliopita au mpiga kura ambae hakuwampiga kura. Kwahiyo, kama ni wazamani ana kadi yake labda iliharibika au kupotea alikuwa anakwenda kuboresha taarifa zake tofauti na Uchaguzi wa Serikali za Mitaa maafisa watakaokuwa wanaandikisha hawatatumia mashine za BVR (Biometric Voters Registration) watakuwa na madaftari ya kusajili wapiga kura” aliongeza Alhaj Shekimweri.

Aidha, alipongeza timu ya Uchaguzi ikiongozwa na Msimamizi wa Uchaguzi Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Dkt. Frederick Sagamiko, kwa kazi nzuri ya uhamasishaji wanayoendelea kuifanya tangu zoezi la kuboresha taarifa katika daftari la kudumu la mpiga kura mpaka sasa kuelekea katika zoezi la kujiandikisha katika orodha ya wapiga kura kwa ajili ya uchaguzi utakaofanyika tarehe 27 Novemba, 2024.




Bonanza la kuhamasisha umma kushiriki katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa liliongozwa na kaulimbiu ‘Serikali za Mitaa, Sauti ya Wananchi, Tujitokeze Kushiriki Uchaguzi’ lilihudhuriwa na watumishi mbalimbali kutoka Ofisi ya Mkuu wa Wilaya, Halmashauri ya Jiji la Dodoma, taasisi mbalimbali na mamia ya wananchi likipambwa na burudani mbalimbali kutoka kwa wanafunzi wa Shule ya Sekondari Dodoma na Chinangali, walimu wa shule za msingi na sekondari, wanamuziki kutoka Dodoma Extra Sound na Dodoma One Theatre. Michezo iliyochezwa ni mpira wa miguu, bao, drafti, kukumbiza kuku, kuvuta kamba, kukimbia na yai pamoja na kukuna nazi.

MWISHO


Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma