Uzinduzi ujenzi jengo la mapumziko Hospitali ya Mkoa wa Dodoma

Na. Asteria Boniface, DODOMA

MBUNGE wa Jimbo la Dodoma mjini, Anthony Mavunde amezindua ujenzi wa jengo la mapumziko la wananchi Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma na kusema kuwa ujenzi huo ni sadaka yake kwa wananchi.




Alisema kuwa nje ya jengo hilo kuna eneo ambalo wanakaa wananchi ambao asilimia kubwa hawaishi katika Jiji la Dodoma na wanatumia sehemu ile kama sehemu ya kupumzikia kwaajili ya kusubiri muda wa kuwaona wagonjwa wao. Aliongeza kuwa wapo baadhi ambao hawana sehemu ya kulala na hawana makazi Dodoma na hawawezi kurudi walipitoka kwasababu ni mbali.

Mbunge huyo alisema kuwa wakati mwingine wakina mama, baba na watoto wanachanganyikana na kulala sehemu moja. Alisema kuwa kulingana na maadili ya kitanzania sio vema sana kuchanganyika watu wa jinsi tofauti sehemu moja na hasa ambao kwa namna moja au nyingine hawana uhusiano wowote. “Mimi kama Mbunge, jambo hili lilinigusa sana nikasema moja ya sadaka, Mungu akinijalia na nitapenda niiache kama alama ni kiwahifadhi na kiwastiri wananchi wangu ambao wanakaa katika eneo lile ambalo lipo wazi. Nikasema nitalifanyia kazi na leo ndugu zangu nimezindua rasmi ujenzi wa jengo la kisasa kabisa na wananchi wa ndani na nje ya Dodoma watapata sehemu nzuri ya kupumzika” alisema Mavunde.

Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma, Dkt. Sara Ludoviki alitoa taarifa fupi kuhusu hospitali hiyo na kueleza changamoto wanazopitia katika baadhi ya majengo yanayotoa huduma hospitalini hapo.

Alisema kuwa hospitali hiyo ina miaka 104 na ilianza kama kituo cha afya na imekua na kufikia hadhi ya kuwa hospitali ya Mkoa kwa tangazo la serikali toleo namba 46 la tarehe 12 Novemba, 2010. Aliongeza kuwa hospitali inatoa huduma kwakupitia sera, miongozo na taratibu zilizowekwa na Wizara ya Afya.  

“Tunamshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutuletea madaktari bingwa 31. Nusu ya madaktari hao, wamepatikana katika awamu hii ya sita. Mafanikio tuliofikia ni kwa upande jengo la uzazi kwa kupunguza vifo vya wamama wajawazito na watoto kwa kuwekwa kwa huduma mbalimbali kama sehemu ya uangalizi wa wagonjwa mahututi ya watoto na pia katika idara ya mionzi tumewekewa ‘CT scan’" alisema Dkt. Ludoviki.




Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma inauwezo wa kuhudumia wagonjwa zaidi ya 1,500 kwa siku moja ambao ni mchanganyiko wa wagonjwa wa nje na walio lazwa na wengine wanaotoka katika mikoa jirani.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma