Ujenzi wa Shule ya Sekondari Miyuji B waweka historia

Na. Mwandishi Wetu,

SERIKALI ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan imeweka historia kwa kujenga Shule ya Sekondari Miyuji B na kuwasaidia wanafunzi waliokuwa wakitembelea umbali mrefu kufuata elimu katika Kata ya Mnadani.

Mwl. Fredrick Mwakisambwe akielezea shule ya Sekondari Miyuji B


Kauli hiyo ilitolewa na mwakilishi wa Mkuu wa Divisheni ya Elimu Sekondari, Mwl. Fredrick Mwakisambwe alipokuwa akiongea na waandishi wa habari waliotembelea shule hiyo kujionea mafanikio ya miaka mitatu ya serikali ya awamu ya sita katika Shule mpya ya Sekondari Miyuji B iliyopo Kata ya Miyuji jijini Dodoma.

Mwl. Mwakisambwe ambae pia Afisa Elimu Vifaa na Takwimu katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma alisema kuwa shule hiyo imekamilika ikianza na wanafunzi wa kidato cha kwanza. “Ni mara ya kwanza katika hitoria ya Kata ya Miyuji kuwa na shule ya sekondari. Watoto wameteseka kwa muda mrefu kutembea umbali mrefu kufuata huduma ya elimu. Tunamshukuru sana mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, mwaka jana 2023 alitupatia shilingi 544,000,000 kujenga shule hii ya kisassa kabisa yenye madarasa nane, maabara tatu, jengo la utawala, jengo la TEHAMA na matundu ya vyoo” alisema Mwl. Mwakisambwe.

Akiongelea mchango wa shule hiyo katika kukuza taaluma, alisema kuwa itasaidia kuongeza kiwango cha ufaulu. “Ni jambo la kipekee kwetu sisi wasimamizi wa elimu katika Jiji la Dodoma kwasababu tulikuwa tukipata shida sana katika usimamizi wa taaluma. Lakini uwepo wa shule hii unaongeza chachu kwa watoto kuweza kusoma vizuri, utoro utapungua na utulivu kwa watoto wetu utakuwepo. Tunamshukuru sana mheshimiwa Rais kwa kipindi hiki cha miaka mitatu katujengea shule nyingi na hii ni moja wapo” alisema Mwl. Mwakisambwe kwa sauti ya shukrani.

Muonekano wa Shule ya Sekondari Miyuji B


Akiongelea faida ya kujengwa Shule mpya ya Sekondari Miyuji B, Mkuu wa Shule hiyo, Mwl. Clara Mwinshehe alisema kuwa ni ukombozi kwa wanafunzi. “Faida ya kujengwa kwa shule hii ni wanafunzi wengi walikuwa wakipata changamoto kutoka eneo hili kwenda Kata ya Mnadani umbali wa kama kilometa saba kutoka hapa. Jambo ambalo lilikuwa linasababisha watoto wakike kushindwa kumaliza masomo kwa changamoto za mimba kutokana na kutembea umbali mrefu. Tunamshukuru sana mheshimiwa Rais kwa kuleta hii shule Mtaa wa Mpamaa, Kata ya Miyuji inawanufaisha wanafunzi na watafanya vizuri zaidi kwenye masomo yao kwasababu imewapunguzia kutembelea umbali mrefu kufuata elimu. Mungu akubariki sana mama, tunakushukuru kwa miaka mitatu, tunakupongeza” alisema Mwl. Mwinshehe kwa furaha.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Mtaa wa Mpamaa, Happy Joshua alisema kuwa shule hiyo ni muhimu kwa wananchi wake. “Napenda kumshukuru mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa mradi huu mkubwa wa shule ya sekondari maana katika Kata ya Miyuji hatukuwa na shule ya sekondari. Pia niwashukuru wananchi wa Mpamaa kwa kujitoa kwao katika mradi huu. Manufaa ya mradi huu ni watoto wetu hawatatembea tena umbali mrefu kufuata elimu” alisema Joshua.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma