Bazara la Madiwani Jiji la Dodoma lapitisha rasimu ya Mpango na Bajeti shilingi 146,287,642,299 kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025


Na. Dennis Gondwe, DODOMA

BARAZA la Madiwani la Halmashauri ya Jiji la Dodoma limepitisha rasimu ya mapendekezo ya Mpango na Bajeti ya mwaka wa fedha 2024/2025 jumla ya shilingi 146,287,642,299.70 ikitajwa kuwa ni bajeti ya wananchi.

Mkuu wa Divisheni ya Mipango na Uratibu, Francis Kaunda akiwasilisha rasimu ya Mpango na Bajeti kwa mwaka wa fedha 2024/2025


Akiwasilisha kwa niaba ya Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma mapendekezo ya rasimu ya Mpango na Bajeti kwa mwaka wa fedha 2024/2025 katika Mkutano wa Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Jiji la Dodoma Mkuu wa Divisheni ya Mipango na Uratibu, Francis Kaunda alisema kuwa bajeti hiyo imelenga kutatua changamoto za wananchi.

“Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo ya rasimu ya Mpango na Bajeti ya Halmasahuri ya Jiji la Dodoma kwa mwaka wa fedha 2024/2025 ni jumla ya shilingi 146,287,642,299.70. Kati ya fedha hizo, shilingi 58,521,926,299.70 ni mapato ya ndani, shilingi 73,852,812,000 ni ruzuku ya mishahara, shilingi 1,168,778,000 ruzuku ya matumizi mengineyo na shilingi 12,744,126,000 ni ruzuku ya miradi ya maendeleo. Hivyo, bajeti ya mwaka wa fedha 2024/2025 imeongezeka kwa 14.4% ukilinganisha na bajeti ya mwaka wa fedha 2023/2024” alisema Kaunda. 

Mwenyekiti wa mkutano huo ambae ni Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Prof. Davis Mwamfupe alisema kuwa bajeti hiyo imemlenga mwananchi wa kawaida moja kwa moja. “Ndiyo maana tukaweka mkazo mkubwa katika sekta ya elimu na sekta ya afya. Mfano katika elimu ya msingi tumeweza kuongeza vyumba vya madarasa 76, katika sekondari maabara 15 zimekamilika mpaka sasa. Katika miradi tumejikita zaidi kuhakikisha miradi viporo ndiyo inakuwa ya kipaumbele ili kuunga juhudi za wananchi katika maeneo ya pembezoni mwa halmashauri yetu” alisema Prof. Mwamfupe.

Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Maduhu Ilanga alisema kuwa timu yake ya wataalam imejipanga vizuri kutekeleza bajeti hiyo. “Mheshimiwa Mwenyekiti nikuhakikishie kwamba tumejipanga, tupo na timu nzuri ya wakuu wa divisheni na vitengo pamoja na watendaji wengine. Bahati nzuri tumejipangia malengo na tumepeana mikataba. Kwa hiyo nikuhakikishie kilichopitishwa na baraza lako na ushauri uliotolewa tutakwenda kuutekeleza kwa weledi mkubwa. Tutakusanya kila shilingi ambayo tumeipitisha kwa weledi. Tutakusanya kwa kuwapa elimu wananchi ili walipe kodi wakielewa haya ndiyo maendeleo yao” alisema Ilanga.

Akichangia katika rasimu hiyo, Diwani wa Kata ya Chang’ombe, Bakari Fundikira aliitaja bajeti hiyo kuwa inagusa wananchi moja kwa moja. “Mimi niwashukuru wataalam wetu kutuandalia rasimu ya bajeti hii nzuri, kupitia vikao vyetu mbalimbali madiwani walishauri maeneo kadhaa na kuelekeza fedha ziende kwenye miradi ya maendeleo inayogusa wananchi moja kwa moja. Kufanya hivyo, tutahakikisha kero katika kata zinatatuliwa katika mwaka wa fedha 2024/2025” alisema Fundikira.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Kilimani, Neema Mwaluko alisema bajeti ni nzuri nakusisitiza ukusanyaji wa mapato ili kuitekeleza bajeti hiyo. “Mheshimiwa Mwenyekiti kupanga bajeti ni kitu kingine na utekelezaji ni kitu kingine. Waswahili wanasema kidole kimoja hakivunji chawa, ili tukaitekeleza bajeti hii vizuri ndugu madiwani na wataalam twende tukaungane ili tuweze kukusanya mapato yatakayoweza kutekeleza bajeti hii” alisisitiza Mwaluko.

 


MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma