KAMATI YA SIASA WILAYA YA DODOMA YAPONGEZA UJENZI KITUO CHA AFYA ILAZO

 

NA. Dennis Gondwe, ILAZO

KAMATI ya Siasa ya Wilaya ya Dodoma imeridhishwa na hatua ya ujenzi wa Kituo cha Afya Ilazo unaoendelea na kusema kuwa wilaya inaoga maendeleo.

Wajumbe wa Kamati ya Siasa Wilaya ya Dodoma wakikagua ujenzi wa Kituo cha Afya Ilazo


Kauli hiyo ilitolewa na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Dodoma, Charles Mamba alipoongoza Kamati ya Siasa Wilaya ya Dodoma kutembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa Kituo cha Afya Ilazo kinachojengwa jijini Dodoma.

Mamba alisema “nianze kwa kumshukuru Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuitendea mema Dodoma hasa Halmashauri ya Jiji la Dodoma. Sisi tunaoga maendeleo. Kata ya Nzuguni, Ipagala na kata za jirani. Mradi huu ni wenu na ni jukumu lenu kuutunza ili uwe endelevu”.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi Wilaya ya Dodoma, Shaban Shaban alisema kuwa wasimamiz wa ujenzi wa Kituo cha Afya Ilazo wapo makini. “Kwa jinsi tulivyoukagua tu mradi tumeona kuta zimenyooka vizuri na msingi umejengwa kwa kiwango bora kabisa. Mheshimiwa Rais, anapotoa fedha anataka kuona zinatumika vizuri. Bila usimamizi mzuri hatuwezi pata kilichokusudiwa. Pongezi kwa usimamizi wako Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, sisi kama vijana tutarudi hapa kwa sababu vijana wa CCM hii ndo miradi ya kutembelea kwenye kata. Umoja wa vijana wa CCM hizi ndizo kazi zetu kusimamia na uadilifu” alisema Shaban.

Akisoma taarifa ya mradi wa ujenzi wa Kituo cha Afya Ilazo, Mwakilishi wa Mkuu wa Divisheni ya Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Goodluck Magoti alisema kuwa lengo la ujenzi wa kituo hicho ni kuboresha huduma za mama na mtoto na huduma za upasuaji.

Mwakilishi wa Mkuu wa Divisheni ya Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Goodluck Magoti


Alisema kuwa jengo la mama na mtoto ujenzi wa lenta umekamilika. “Jengo la wagonjwa wa nje jamvi limekamilika hatua ya kupandisha kuta inafuata. Jengo la Maabara lipo kwenye hatua ya kufunga lenta. Jengo la wodi ya wazazi, jamvi limekamilika hatua inayofuata ni kupandisha kuta. Majengo mengine ni la upasuaji lipo kwenye hatua ya upangaji mawe. Jengo la kuhifadhia maiti lipo kwenye hatua ya lenta na jengo la kufulia lipo kwenye hatua ya lenta” alisema Magoti.

Aliongeza kuwa halmashauri imepokea baadhi ya vifaa tiba kwa ajili ya kituo hicho. Alivitaja vifaa hivyo kuwa ni vifaa vya chumba cha upasuaji na majenereta mawili.

Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri akisisitiza jambo

Nae Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri alisema kuwa kituo hicho kitakuwa kikubwa chenye hadhi ya hospitali ya wilaya. Alisema kuwa ujenzi wa kituo hicho ni matokeo ya ziara za Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan nje ya nchi na kukuza diplomasia ya kiuchumi.


Ikumbukwe kuwa Kituo cha Afya Ilazo kinajengwa na Mkandarasi Salem Construction Ltd kwa gharama ya shilingi 2,800,000,000 chini ya ufadhili wa KOICA kupitia Shirika la kuhudumia Watoto UNICEF kikitarajia kuhudumia wananchi 99,743 wa Kata ya Nzuguni na Ipagala.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma