KAMATI YA SIASA KATA YA MSALATO YATAKIWA KUSIMAMIA MIRADI

 

Na. Dennis Gondwe, MSALATO

KAMATI ya Siasa ya Kata ya Msalato imetakiwa kufuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika kata ili kujiridhisha ya thamani ya fedha.

Kauli hiyo ilitolewa na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Dodoma, Charles Mamba alipoongoza Kamati ya Siasa Wilaya ya Dodoma kutembelea na kukagua ujenzi wa mabweni mawili, vyumba saba vya madarasa na matundu 10 ya vyoo katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Msalato iliyopo Kata ya Msalato jijini hapa.

Mamba alisema kuwa Kamati ya Siasa Kata ya Msalato ina wajibu wa kufuatilia na kusimamia miradi yote ya maendeleo inayotekelzwa katika kata hiyo. “Kamati ya Siasa Kata ya Msalato mradi huu ni wa kwenu, msisubiri Kamati ya Siasa Wilaya ya Dodoma kuja kukagua. Lazima muwe mnapanga ratiba zenu kukagua miradi hii. Serikali ya awamu ya sita inaleta fedha nyingi kwenye kata kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo, jukumu lenu ni kusimamia utekelezaji wake na thamani ya fedha ionekane katika miradi hiyo” alisema Mamba kwa msisitizo.

Akisoma taarifa ya ujenzi wa mabweni mawili, vyumba saba vya madarasa na matundu 10 ya vyoo kwa Kamati ya Siasa Wilaya ya Dodoma Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Wasichana Msalato, Mwl. Mwasiti Msokola alisema kuwa shule yake ilipokea shilingi 428,000,000 kutoka serikali kuu. “Fedha hizo zilikuja kwa ajili ya ujenzi wa mabweni mawili, vyumba saba vya madarasa na matundu 10 ya vyoo. Lengo la mradi huu ni maandalizi ya kuwapokea wanafunzi 452 wa kidato cha tano mwaka 2023. Ujenzi huu unatekelezwa kwa kutumia utaratibu wa ‘force account’ ambapo kamati tatu ziliundwa za ujenzi, manunuzi na mapokezi ili kusimamia utekelezaji wa mradi huu” alisema Mwl. Msokola.

Mkuu huyo wa shule alimshukuru Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwapatia fedha hizo kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu. “Miundombinu hii itasaidia kupunguza upungufu wa mabweni, madarasa na matundu ya vyoo shuleni hapa. Kipekee tunatoa shukrani za dhati kwa ushirikiano wa karibu wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Kamati ya Usalama Wilaya chini ya Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Ofisi ya Mkurugenzi wa Jiji pamoja na uongozi wa Kata ya Msalato, walimu wote na kamati za utekelezaji mradi huu” aliongeza.




Awali akimkaribisha Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Dodoma, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaj Jabir Shekimweri alisema kuwa Shule ya Wasichana Msalato ni shule maalum inayochukua wanafunzi na walimu wenye vipaji toka nchi nzima. “Tunaendelea kuwapa nguvu na kuwatia moyo Shule ya Sekondari ya Sasichana Msalato kwa sababu wilaya tunawategemea kwenye ufaulu na kuipaisha Wilaya ya Dodoma” alisema Alhaj Shekimweri.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma