MAKARANI UCHAGUZI MDOGO KATA YA NALA WAHIMIZWA UADILIFU

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

MAKARANI wa vituo vya kupigia kura katika uchaguzi mdogo wa udiwani wa Kata ya Nala, Halmashauri ya Jiji la Dodoma wametakiwa kufanya kazi kwa uadilifu ili kufanikisha uchaguzi huo.

Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Dodoma mjini, John Kayombo


Kauli hiyo ilitolewa na Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Dodoma mjini, John Kayombo alipokuwa akifungua mafunzo kwa makarani wa vituo vya kupigia kura katika uchaguzi mdogo wa Kata ya Nala yaliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma.

Kayombo ambae pia ni Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma alisema “ninyi makarani tumewaamini, tumewapa ridhaa muende mkafanye kazi hiyo kwa uadilifu mkubwa kabisa. Wakati tunawachagua tuliangalia sifa zenu, mliomba wengi. Mheshimiwa Jaji waliomba watu 1,500 lakini kupata hawa 12 ni mchakato ambao tumeufanya usiku na mchana mpaka kupata hawa 12 na wa akiba wawili. Siyo kwamba wale wengine hawana sifa hapana. Sifa moja wapo lazima awe raia wa Taznania, awe muadilifu, mvumilivu, mwenye hekima, busara, msikivu na anayeweza kufanya kazi kwa kujituma, tunaamini haya mtakwenda kuyazingatia”.

Akiongelea kiapo, Kayombo alisema “mmekula kiapo na kwenye zile sifa tumesema asiwe mshabiki wa chama cha siasa. Chama chako umeshakiacha huko, usiende kushabikia chama cha siasa, umeshakula kiapo cha kujitoa kwenye chama cha siasa. Umekula kiapo cha kutunza siri hayo yamekwisha, chochote utakachokwenda kuona kule ni siri yako, wewe sasa ni mtumishi wa Tume. Kazi yenu nyingine ni kwenda kuwasaidia wale wapiga kura bila upendeleo wowote wala ubaguzi”.

Kwa upande wake Mjumbe wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Mahakama ya Rufaa, Mhe. Mwanaisha Kwariko aliwataka makarani hao kutunza viapo vyao. “Hapa mmekula kiapo, ina maana usipotekeleza yale ambayo umeelekezwa kutekeleza kile kiapo chako kinaweza kwenda kukufunga. Kwamba umekosea hapa na wakati uliapa utatekeleza hivi, kwa hiyo unaweza kushitakiwa kwa kile kiapo ulichoahidi na kushindwa kukitekeleza” alisema Mhe. Jaji Kwariko.

Mjumbe wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Mahakama ya Rufaa, Mhe. Mwanaisha Kwariko


Aidha, aliwataka kutokufanya kazi kwa mazoea. Aliwataka kuona kuwa kila unapofanyika uchaguzi wajue ni tukio jipya na kuepuka kufanya kazi kwa mazoea. “Wapiga kura ndio wateja wetu wa siku hiyo, mteja inatakiwa umpe huduma nzuri, mteja ni mfalme kwahiyo, wale wapiga kura ni wateja wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwa hiyo tunatarajia kufanya kazi kwa weledi” alisema Mhe. Jaji Kwariko.

Mafunzo kwa makarani 12 wa vituo vya kupigia kura katika uchaguzi mdogo wa udiwani Kata ya Nala yalitolewa ikiwa ni maandalizi kuelekea uchaguzi huo utakaofanyika tarehe 19 Septemba, 2023.

 


MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma