KAMATI YA UJENZI, MANUNUZI NA MAPOKEZI JIJI LA DODOMA ZATAKIWA KUWA NA WATAALAM

Na. Dennis Gondwe, MIYUJI

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, John Kayombo ameagiza kamati zinazohusika na ujenzi, manunuzi na mapokezi ya vifaa kuwa na wataalam wa fani husika ili kwenda sawa na matakwa ya mwongozo wa matumizi ya ‘force account’ katika kutekeleza miradi ya ujenzi.



Agizo hilo alilitoa alipotembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa shule mpya ya Sekondari Miyuji inayojengwa katika Kata ya Miyuji jijini Dodoma.

Kayombo alisema kuwa mwongozo wa matumizi ya ‘force account’ unaelekeza ziundwe kamati zenye mchanganyiko wa wajumbe na wataalam. Kamati hizo ni ujenzi, manunuzi na mapokezi ya vifaa. “Katibu wa Kamati ya Manunuzi lazima awe mtaalam wa Manunuzi. Lengo ni kuwaongoza wajumbe kwenye taratibu za Manunuzi kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizopo. Kamati ya Ujenzi katibu wake anatakiwa kuwa Mhandisi na Kamati ya Mapokezi inatakiwa kuwa na mtu mwenye ujuzi wa mapokezi na utunzaji wa vifaa. Hivyo, maelekezo yangu wataalam hao waingizwe kwenye kamati ili kamati iwe na ufanisi katika kutekeleza majukumu yake” alisema Kayombo.

Aidha, alisema kuwa tafsiri sahihi ya kujenga ni pamoja na kutunza taarifa sahihi za mradi. “Naelekeza kamati za maendeleo zipewe taarifa sahihi na kufikia tarehe 30 Septemba, 2023 mradi huu ukabidhiwe ukiwa umekamilika” alisisitiza Kayombo.

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Miyuji, Beatrice Ngerangera alisema kuwa dhamira ya serikali kujenga shule hiyo mpya ni kuwasaidia watoto wanaotembea umbali mrefu kufuata shule ili waweze kusoma karibu. “Mimi lengo lango kwa huu mradi ufike hatua ambayo Rais, Dkt. Samia anataka kwa sababu ni mradi mkubwa na ni zawadi kwa wananchi wangu wa Kata ya Miyuji. Watoto wanaotoka huku kwenda kusoma Miyuji ni mbali sana. Kwa hiyo ninatamani hii shule ikamilike mapema ikiwezekana mwezi Oktoba watoto wanaosoma kule Miyuji waje kuanza kusoma hapa ndiyo nia yangu na lengo langu kubwa wananchi wangu wa Miyuji” alisema Ngerangera.

Awali Mkuu wa Shule ya Sekondari Miyuji, Greyson Maige alisema kuwa shule yake ilipokea kiasi cha shilingi 544,225,626 kutoka mradi wa kuboresha ubora wa elimu ya sekondari nchini (SEQUIP) kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya ya sekondari Miyuji.

Akiongelea hatua za utekelezaji wa mradi huo alisema kuwa ujenzi wa madarasa mawili yapo hatua ya ujenzi wa kuta na mawili yapo hatua ya kumwaga jamvi. “Ujenzi wa madarasa manne yenye ofisi mbili ni darasa moja lipo kwenye hatua ya kupaua na madarasa matatu yapo kwenye hatua ya kuweka renta. Jengo la utawala tulitenga siku mbili kwa ajili ya kumwagilia maji na sasa lipo katika hatua ya ujenzi wa renta ambao unaendeleo leo. Jengo la maabadara ya kemia na baiolojia lipo hatua ya ujenzi wa renta” alisema Maige.

Majengo mengine aliyataja kuwa ni maabara ya fizikia iliyopo hatua ya kupanga mawe katika msingi. “Jengo la maktaba lipo katika hatua ya ujenzi wa renta. Jengo la Tehama lipo hatua ya ujenzi wa renta. Jengo la vyoo vya wasichana hatua ya kumwaga jamvi” alisema.

 

MWISHO  

 

 

 

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma