CHANG’OMBE WATAKIWA KUSAFISHA MAZINGIRA KUZUIA WAHALIFU

Na. Dennis Gondwe,

WAKAZI wa Kata ya Chang’ombe wametakiwa kudumisha usafi wa mazingira kwa lengo la kuzuia maficho ya wahalifu na kulinda afya zao ili waweze kufanya shughuli za kujitelea maendeleo.



Kauli hiyo ilitolewa na Afisa Mtendaji wa Kata ya Chang’ombe, Tunu Dachi alipoongoza uzinduzi wa kampenzi ya usafi wa mazimgira katika kata hiyo tukio lililofanyika katika Mtaa wa Mazengo jijini Dodoma.

Dachi alisema “nilipofika Kata ya Chang’ombe niligundua kuwa kata yetu ni chafu sana. Na katika kufanya vikao na wadau wa usafi wa mazingira tulikubaliana kuwa Mtaa wa Mazengo ndio mtaa mchafu kuliko mitaa yote. Leo nataka tushirikishane jambo rahisi sana, vikundi vya uzoaji taka vimeridhia kwamba kila Jumamosi wataungana kwa umoja wao na jamii ya mtaa husika kuja kufanya usafi wa maeneo ambayo mwenyekiti atakuwa amependekeza”.

Aliwataka wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki katika mazoezi ya usafi wa mazingira kila siku ya Jumamosi. “Kwa hiyo, mwananchi akisema anaenda kumfanyia mtu usafi, hapana hatumfanyii mtu usafi tunajifanyia sote usafi. Jirani yako akiwa msafi na wewe umesalimika, wewe ukiwa msafi na jirani yako amesalimika. Kutupa taka ovyo ndio tunazalisha maficho ya vibaka na wavuta bangi. Sera yangu nataka Kata ya Chang’ombe iwe safi na salama. Ulinzi na usalama unaanza kwenye usafi wa mazingira” alisema Dachi.

Akiongelea tabia ya baadhi ya wananchi kukaidi kujitokeza kushiriki mazoezi ya usafi wa pamoja siku ya Jumamosi alisema kuwa wananchi wote wanatakiwa kujitokeza kushiriki kufanya usafi. “Mwananchi kutoka kushiriki zoezi la usafi ni suala la lazima siyo hiyari. Mwananchi atakayekiuka utekelezaji wa zoezi la usafi faini yake ni shilingi 50,000. Leo tunapeana elimu Jumamosi ijayo tunatekeleza na tutakayemkuta na makosa ya ziada faini inaenda mpaka shilingi 300,000. Tujipende sisi na tuwapende jirani zetu. Mwananchi anayeelewa thamani ya afya hawezi kugomea usafi, mkiwa wasafi maradhi yataondoka na kipato chenu kitatumika kwa shughuli za maendeleo” alisema Dachi kwa msisitizo.

Alisema kuwa zoezi hilo la usafi ni endelevu kwa mitaa yote ya kata hiyo. “Usafi siyo suala la zimamoto, nataka Chang’ombe iwe safi. Halmashauri ya Jiji la Dodoma inatoa vyeti, vifaa vya usafi kwa mtaa msafi na fedha zinatolewa hadi shilingi 8,000,000 za kutekeleza miradi ya maendeleo. Hivyo, kila mtu afanye usafi mita tano kuzunguka nyumba yake” alisema Dachi akionesha matumaini ya mmoja ya mitaa yake kuibuka mshindi wa usafi.

Kwa upande wake, Jumanne Mwema alisema kuwa Chang’ombe inahitaji msisitizo mkubwa katika usafi wa mazingira. “Alichosema huyu mama ni ukweli. Pita kwenye mitaa utakuta uchafu umetakapaa, watoto wanacheza kwenye uchafu. Nimefurahi alipooanisha usafi na afya za wananchi labda msisitizo ukiwekwa hapo watu wanaweza kubadilika na kupenda kukaa na kufanya kazi kwenye mazingira safi” alisema Mwema.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma