Lishe bora yahamasishwa Kliniki ya Magonjwa Yasiyoambukiza Nyerere Square
Na. Nancy Kivuyo, DODOMA
Mamia
ya wananchi wamejitokeza kupima afya zao katika kliniki maalum ya magonjwa
yasiyoambukiza ikiwa ni sehemu ya kampeni ya kuongeza uelewa kuhusu uchunguzi
wa mapema, lishe bora na kuzuia magonjwa yanayoendelea kuongezeka nchini.
Taarifa
hiyo ilitolewa na Daktari Bingwa wa Afya ya Jamii, Dr. Peter Daud alipokuwa
akizungumza na waandishi wa habari katika bustani ya mapumziko Nyerere Square
ambapo maadhimisho ya wiki ya Upimaji Magonjwa yasiyoambukiza yakitamatika.
Dr.
Daud alisema kuwa mwamko mkubwa ulioonekana ni ishara kuwa elimu ya lishe na
uchunguzi wa mapema inawafikia wananchi kwa ufanisi.
“Sehemu kubwa ya magonjwa yasiyoambukiza inahusiana na lishe. Tunawahimiza
wananchi kupunguza vyakula vyenye mafuta mengi, kula kwa uwiano sahihi na
kufanya mazoezi. Hii ni kinga muhimu sana” alisema Dr. Daud.
Aliongeza
kwa kutoa wito kuwa wananchi waache tabia bwete kwa kuhakikisha wanafanya
mazoezi, kutembea umbali mdogo kwaajili ya kuweka mwili na misuli timamu ili
kukwepa maradhi yasiyo ya lazima.
Kwa
upande wake, Afisa Muuguzi kutoka Kituo cha Afya Makole, Mwendwa Galahenga
alisema kuwa kliniki za wazi kama hizo zinawapa wananchi fursa ya kupata elimu
ya lishe kila wanapoenda kupima.
“Watu wengi leo wamegundua kuwa ongezeko la uzito na shinikizo la damu
linatokana na ulaji usio sahihi. Tunawaelekeza nini kile wanachopaswa
kubadilisha kwenye mlo wa kila siku ili wawe na uzito sahihi. Ni jukumu letu
sisi wataalam lakini pia wananchi kuwa na mazoea ya kutembelea hospitali, vituo
vya afya, kiliniki kama hizi kwasababu watajifunza mambo mzuri na yenye tija
kuhusiana na lishe bora” alieleza.
Katika
hatua nyingine, Dr. Zaituni Mgaza, Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Wanawake
alisema kuwa upatikanaji wa elimu ya lishe ni nguzo muhimu katika kupunguza
hatari ya saratani na magonjwa mengine kwa wanawake. “Lishe bora ni ngao ya
kwanza ya afya. Wanawake wakipata elimu sahihi kuhusu nini wanapaswa kula, muda
gani wale na namna ya kuchagua vyakula salama tunapunguza maradufu hatari za
magonjwa yanayoweza kuzuilika” alisema.
Miongoni
mwa waliopata huduma, Joyce Wikezi aliyefanyiwa uchunguzi wa saratani ya matiti
na mlango wa kizazi alisema kuwa kliniki hiyo imempa nafasi ya kujitokeza
kupima magonjwa hayo kabla hajaenda kwenye ngazi zingine. “Nimepata pia elimu
ya lishe, jambo ambalo sikuwahi kulielewa vizuri. Wamenifundisha umuhimu wa
kula kwa uwiano na kuepuka vyakula vinavyoongeza hatari ya saratani.
Nimejifunza mengi” alisema Joyce kwa shukrani.
Kliniki
hiyo ilianza tangu tarehe 12 Novemba na kuhitimishwa leo tarehe 14 Novemba,
2025 ambapo wananchi wamepata fursa ya kupima shinikizo la damu, kiwango cha
sukari, uzito na urefu, uchunguzi wa magonjwa ya moyo pamoja na ushauri wa kina
kuhusu lishe ikiwa ni pamoja na matumizi sahihi ya mbogamboga, matunda, ulaji
wa vyakula visivyo na mafuta mengi, pamoja na kupunguza sukari na chumvi.
MWISHO
Comments
Post a Comment