Watahiniwa 19,176 Darasa IV kupimwa Jiji la Dodoma

Na. Nancy Kivuyo, DODOMA

Maandalizi ya Mtihani wa Upimaji Kitaifa kwa Darasa la Nne (SFNA) utakaofanyika tarehe 22-23 Oktoba, 2025 yamekamilika ambapo Halmashauri ya Jiji la Dodoma yenye shule 174 kati ya shule 188 za msingi zitashiriki kufanya mtihani huo.



Mkuu wa Divisheni ya Elimu ya Awali na Msingi, Mwl. Prisca Myalla alisema kuwa kati ya watahiniwa 19,176 wasichana ni 9,654 sawa na asilimia 50.4 huku wavulana wakiwa 9,522 ambao sawa na asilimia 49.6

Aliongeza kuwa maandalizi yote yamekamilika na miundombinu ni rafiki kwa watahiniwa wote. “Maandalizi yamekamilika, tunasubiri muda ufike ili watahiniwa wetu wafanye mitihani yao vizuri bila changamoto yoyote. Vituo vyote vitakavyotumiwa ni salama kabisa kwa mantiki hiyo niwakumbushe wazazi kuwaandaa watahiniwa vizuri lakini pia nao walengwa wajiandae” alisema Mwl. Myalla.

Nae, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Dkt. Frederick Sagamiko aliwatakia heri na baraka watahiniwa wote wa mtihani huo. Aidha, aliwataka walimu kutekeleza jukumu la kitaifa kwa kuzingatia sheria, kanuni, taratibu na miongozo iliyopo ili kulifanya zoezi hilo kukamilika kwa weledi.



Shule 14 ambazo hazitashiriki katika mtihani huo ni shule zenye madarasa ya awali na shikizi ambazo zilijengwa karibu na makazi ya wananchi ili kuwapunguzia wanafunzi kutembea umbali mrefu kufuata elimu.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Agenda ya Lishe yaongeza Ari ya usomaji S/M Dodoma Makulu

Wananchi watakiwa kuwa msitari wa mbele kupinga ukatili

SERIKALI YAPONGEZWA KUTOA FEDHA UJENZI WA DODOMA ENGLISH MEDIUM