Wanafunzi Hazina Sec watakiwa kufunguka dhidi ya ukatili

Na. Halima Majidi, HAZINA

Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Hazina, iliopo katika Kata ya Hazina, Halmashauri ya Jiji la Dodoma, wametakiwa kuwa wawazi na wakweli katika kuripoti matukio ya ukatili wa kijinsia ili kuepuka vitendo hatarishi vitakavyo sababisha kudumaza fikra na ufaulu katika masomo yao.


Hayo yalisemwa na Afisa Mtendeji wa Kata ya Hazina, Tunu Dachi alipofanya ziara ya utoaji wa elimu juu ya masuala mbalimbali katika kata hiyo.

Alisema kuwa inabidi ziara zifanyike mara kwa mara za kutoa elimu ili watoto wetu waweze kujitambua waelewe majukumu yao wakiwa shuleni, waweze kusoma katika mazingira mazuri kiakili na kihisia. “Leo tumekuja shuleni kama 'normal routine' kwaajili ya kuwatembelea watoto, kuwapa elimu dhidi ya ukatili kwa ujumla, watoto wamekuwa wakweli wameuliza maswali ambayo sisi yametupa kazi ya kwenda kuyafanyia kazi na kuwaletea majibu chanya’ alisema Dachi.

Alisema kuwa, anaamini ili mwanafunzi afanye vizuri sio mpaka awe na majengo na walimu wazuri ila awe tayari kupokea kile anachofundishwa. “Tumefurahi sana na tumefarijika sana watoto wetu wa shule ya Sekondari  Hazina ni weledi wamechangia mada, wameuliza  maswali tumepata kufungukiwa mambo mengi ambayo na sisi yametugusa kama walezi wao wa kata” alisema Dachi.

Aidha, alifafanua kuwa kuhusu masuala ya ulinzi na usalama yeye kama Mwenyekiti wa Kamati hiyo atahakikisha usalama wao unaimarika hasa katika mazingira ya shuleni ili waweza kufikia malengo yao. “Naahidi kuwalinda, usalama wenu utakuwa wa uhakika, endeleeni kushirikiana nasi pale mtakapopata changamoto ambazo mnahisi haziwezi kupatiwa ufumbuzi hapa shuleni basi zifikisheni ofisini kwetu. Mimi na idara yangu ya maendeleo ya jamii na wataalamu wote tutawapa ushirikiano mtakaouhitaji” alifafanua Dachi.

Nae, Afisa Maendeleo ya Jamii Kata ya Hazina, Sikujua Mkita, alisema kuwa umuhimu wa kutoa elimu hiyo ni kuwawezesha watoto kujitambua na kuweza kugundua ukatili wa kijinsia wanaoweza kufanyiwa. “Kuna ukatili wa aina mbalimbali, na watoto wanafanyiwa ukati nyumbani, njiani na shuleni, kuna wengine hawawezi kuongea kwenye hadhara. Hivyo, tumeunda baraza shuleni ili watoto waweze kuwa huru kuripoti vitendo vya ukatili bila kuhofia mtu yoyote” alisema Mkita.

Kwa upande wake Mwalimu wa Nidhamu Shule ya Sekondari Hazina, Silvanus Rwechungura, alipongeza wadau akiwemo Afisa Mtendaji Kata kwa kuwatembelea na kuwapatia elimu hiyo na kama shule bado tunaendelea na malezi kwa vijana na pia tunashukuru wadau wa elimu Dodoma, kwa kutambua mchango wetu na tumeweza kupata cheti cha ufaulu wa kidato cha Nne kwa mwaka 2024. “Binafsi kama walimu wa Hazina Sekondari  tumefurahi  sana kwa namna ambavyo wadau wa elimu wametambua mchango wetu, kwa kuangalia cheti kile tumeweza kutoka nafasi ya 53 Wilaya ya Dodoma mwaka 2023, na kufikia nafasi ya 32 mwaka 2024. Huu ni mchango mkubwa kwa wadau kwa namna ambavyo wanatupa ushirikiano  lakini  pia kwa serikali ya awamu ya sita ambayo imeendelea kutoa mchango  mkubwa kwa kuwezesha katika mahitaji mbalimbali” alipongeza Rwechungura.

Atka Kassim ambae ni Mwanafunzi wa kidato cha Nne, katika Shule ya Sekondari Hazina, alisema kuwa anashukuru kwa elimu dhidi ya ukatili wa kijinsia, ambayo itawasaidi kutoa changamoto zinazowakabili. “Tunashukuru kwa elimu hii kwasababu ukatili wa kijinsia katika shule za 'public' huwa ni mkubwa. Hivyo, inatusaidia kutoa yaliopo moyoni mwetu ambapo tunashindwa kuwaambia walimu, tunawaambia nyinyi ili muweze kutusaidia kuepuka janga hili la ukatili wa kijinsia” alisema Kassim.

Mohammedi Naibu Mwanafunzi wa kidato cha tatu, Shule ya Sekondari Hazina, alisema kuwa mbali na elimu hiyo lakini pia tunaomba kujengewa maabara, tunashindwa kufanya majaribio kwa vitendo kwa sababu hatuna maabara. “Maabara imekuwa ni changamoto kubwa, hasa tunaosoma sayansi tunashindwa kufanya vizuri kwasababu hatuna vifaaa hivyo, tunaomba mtusaidie” alisema Naibu.

MWISHO

 

 

Comments

Popular Posts

Mbunge Mavunde akabidhi Kompyuta kwa Kata 41 za Jiji la Dodoma

Wafanyabiashara wa Soko Kuu la Majengo Dodoma watarajia makubwa Mradi wa TACTIC

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma