Wananchi jijini Dodoma watarajia makubwa Kliniki ya Ardhi

Na. Halima Majidi, VIWANDANI

Halmashauri ya Jiji la Dodoma imefanya Kliniki ya Ardhi ambayo inalenga kutatua changamoto za Ardhi zinazowakabili wananchi.




Akizungumza na waandishi wa habari katika kliniki hiyo iliofanyi viwanja vya Manispaa ya zamani, Sara Kashaji ambae ni Mkazi wa Kata ya Ipagala, alisema kuwa awali alikuwa na shamba heka mbili ukanda wa kijani, ambapo alikuwa anafanya shughuli za kilimo, shamba hilo lilichukuliwa na Halmashauri ya Jiji la Dodoma na kuahidiwa kupatiwa eneo lingine kwaajili ya kuendeleza shughuli zake za kilimo.

“Halmashauri walikuja kupima shamba langu, baada ya zoezi la upimaji waliahidi kutupatia maeneo wakazi wa eneo hilo, baada ya hapo tulihama na kuachia vijiji vile na kwenda sehemu nyingine, Kamishna alisema mashamba yale kuna watu wamepewa. Hivyo, sisi tusubiri kupimiwa eneo lingine Kikombo ambapo tulivyofika kule wananchi walikataa maeneo hayo, tukaambiwa tusubiri kupimiwa Makulu na mpaka sasa sijapata ufumbuzi” alisema Kashaji.

Aidha, alifafanua kuwa kero yake kubwa ni kurudishiwa maeneo yake kwa sababu ni muda mrefu tangu ameanza kufuatilia shamba hilo. Alimuomba Kamishna wa Ardhi awaangalie kwa jicho la huruma. “Nimehangaika kwa miaka mingi tangu niahidiwe kupewa mbadala wa shamba lile na tumekuwa tukiahidiwa kupimiwa maeneo hayo lakini mpaka sasa sijapata muafaka” alifafanua Kashaji.

Aliongeza kuwa kutokana na Kliniki ya Ardhi, anatarajia kupata ufumbuzi wa changamoto yake kwa kupatiwa eneo lingine kwaajili ya kuendeleza shughuli zake za kilimo ili kuweza kujikwamia kimaisha na kukuza uchumi wa nchi kwa ujumla. “Mpaka sasa tunatembea hatujapata majibu tunaambiwa bado wanapima. Leo tumetegemea kumkuta kamishna ili tumpatie karatasi zetu kwaajili ya kupata viwanja vyetu, hayo ndio matarajio yangu” aliongeza Kashaji.

Kwa upande wake Selina Mkami, Mkazi wa Kata ya Ipagala alisema kuwa kwa mara ya kwanza alivyoenda na mpimaji alipata matumaini ya kupata eneo lake lakini chakusikitisha hadi leo   bado anahangaika. Hivyo, anaomba mamlaka husika itutae changamoto hiyo. “Nimetembea na nimehangaika kwa muda mrefu bila kukata tamaa ili kuona napata eneo langu, na kinachonisikitisha zaidi nikwamba sisi tulitolewa kwenye maeneo yetu na tukaacha kulima wakawekwa watu wengine kwa kweli inaniuma sana” alisema Mkami.

Nae Msimamizi wa Upimaji wa Ardhi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Hassan Muhsin alisema kuwa ili waweze kuhudumia wananchi kwa pamoja waliona upo umuhimu wakuandaa kliniki hiyo kwa kuhakikisha wananchi wanapata ufumbuzi katika masuala ya Ardhi. “Kwa kushirikiana na vitengo husika leo tutahakikisha kila mwananchi anapata huduma stahiki na tunashukuru wananchi wameonesha muitikio na niwaombe wananchi wawe wawazi, wakweli na uthibitisho. Sisi tumejipanga vizuri katika kuhakikisha tunatatua matatizo yao” alisema Muhsin.

Kliniki ya Ardhi Halmashauri ya Jiji la DOdoma imeanza tarehe 25 na itaendelea hadi tarehe 28 Februari 2025, ikiwa na lengo la kutatua changamoto za ardhi zinazowakabili wananchi.

MWISHO

 

 

Comments

Popular Posts

Mbunge Mavunde akabidhi Kompyuta kwa Kata 41 za Jiji la Dodoma

Wafanyabiashara wa Soko Kuu la Majengo Dodoma watarajia makubwa Mradi wa TACTIC

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma