Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma


Na. Aisha Ibrahim, DODOMA

Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Greyson Msigwa, amesema mradi wa ujenzi wa uwanja wa mpira wa miguu Dodoma, utakaoweza kubeba watu 32,000 ambao utagharimu kiasi cha shilingi bilioni 352 fedha za kitanzania, unatarajiwa kukamilika ndani ya miezi 24, chini ya serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.



Aliyasema hayo katika hafla ya utiaji saini mkataba wa ujenzi wa uwanja wa mpira wa miguu Dodoma, uliohusisha wizara hiyo na Kampuni ya Lemonta SPA, iliofanyika kiwanja cha Changamani, Kata ya Nzuguni, jijini Dodoma.

Akizungumza kuhusu lengo la ujenzi wa uwanja huo, Msigwa alisema, mradi huo ni fursa kwa maendeleo ya michezo kwa wakazi wa Jiji la Dodoma kwasababu uwanja huo utatumika katika mashindano mbalimbali kitaifa na kimataifa ili kuhakikisha sekta ya michezo inazidi kukua.

“Mradi huu ni fursa kwa maendeleo ya wakazi wa Dodoma lakini ni fursa kubwa kwa wanamichezo katika kukuza vipaji vyao, na sisi kama wizara tumejipanga ili uwanja huu utumike kwa mashindano mbalimbali ya kitaifa na kimataifa” alisema Msigwa.

Aidha, aliahidi kuwa atahakikisha wanasimamia mradi huo kwa umakini wa hali ya juu mpaka pale utakapo kamilika ikiwa ni kuunga mkono juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.

“Mheshimiwa waziri, naomba kutoa ahadi mbele yako na mbele ya watanzania, sisi watendaji wako tutasimamia mradi huu hatua kwa hatua, kucha kwa kucha mpaka ukamilike” alisema Msigwa.

Pia, aliipongeza serikali ya awamu ya sita chini ya utawala wa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa juhudi na kazi nzuri inayoendelea kufanyika kwa kuhakikisha mradi huo unashughulikiwa ipasavyo mpaka kukamilika.

Nae, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule, alisema kuwa Dodoma inajivunia kuwa na vivutio vingi vya utalii ikiwa ni pamoja na utalii wa michezo mbalimbali ikiwemo mpira wa miguu ambapo ilikuwa ni ndoto ya muda mrefu ya wakazi wa maeneo yote ya Jiji la Dodoma kuwa na uwanja mzuri wenye viwango vya hali ya juu.

“Moja ya kipaumbele ni Dodoma kuwa mkoa wa utalii na utalii huo ni pamoja na michezo ya mpira wa miguu na tunaishi kwa imani kuwa uwanja huo utakamilika hivyo tujipange kuwa utalii wa michezo utakuwa ni tija kwa wananchi wa Mkoa wa Dodoma” alisema Senyamule.

Sambamba na hayo, aliongeza kuwa matarajio ya kila mkazi wa Jiji la Dodoma, ni kuona mechi za AFCON zakichezwa katika uwanja huo ikiwa ni njia mojawapo ya kukuza sekta ya michezo kitaifa na kimataifa.

“Tumekuwa tukisema kwa wananchi kuwa Dodoma, AFCON itachezwa iwe kwa mechi au kwa mazoezi lakini tunatamani matone ya AFCON yatudondokee hapa Dodoma na ndio maana wananchi kila siku wakawa wanasema hivi kweli!! uwanja upo? Yaani wanaanza kuona kama AFCON haitowahusu” alisema Senyamule.

Alimaliza kwa kusema kuwa wakazi wa Dodoma wapo tayari kushirikiana na Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ili kuhakikisha ujenzi wa mradi huo unatimia kwa wakati maalum uliopangwa.

MWISHO

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma