Wananchi washauriwa kusikiliza elimu na hamasa ya Dodoma Jiji Mtaa kwa Mtaa Uchaguzi Festival

Na. Asteria Frank, DODOMA

Wananchi wameshauriwa kujitokeza kwa wingi kusikiliza elimu inayotolewa na wahamasishaji kutoka Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa njia mbalimbali ikiwemo kikundi maalum cha ngoma cha Dodoma Jiji Mtaa kwa Mtaa Uchaguzi Festival.



Afisa Utamaduni wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Desdery Kuzenza akihamasisha mamia ya wananchi wa Swaswa Mnarani


Hayo, yalisemwa na Afisa Utamaduni wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Desdery Kuzenza alipokuwa akihamasisha wananchi kujitokeza kutumia haki yao ya msingi na ya kikatiba ya kupiga kura na kuwachagua viongozi watakaowafaa kwa manufaa ya maendeleo ya mitaa yao. “Naomba nitoe rai kwa wakazi wa Dodoma na  maeneo mbalimbali waendelee kushiriki  katika ‘program’ mbalimbali za elimu kwa umma ambazo zinalenga kuwaelimisha kuhusiana na umuhimu wa Uchaguzi wa Serikali za Mitaa na nafasi za uongozi wa serikali za mitaa katika maisha yao ya kila siku na tunasema kwamba serikali za mitaa kwa sauti ya wananchi. Hivyo, wajitokeze kupiga kura kwa maendeleo ya mitaa yao na karibuni kushiriki katika tamasha hili la Dodoma Jiji Mtaa kwa Mtaa Uchaguzi Festival” alisema Kuzenza.

Aidha, mmoja wa wasanii katika kikundi cha DOTI, Salum Ramadhani alisema jukumu lao kubwa ni kuwaelimisha wananchi kuhusiana na Uchaguzi wa Serikali za Mitaa hususani tarehe 27 Novemba, 2024 wajitokeze kwa wingi kwenye kupiga kura kwaajili ya kumchagua kiongozi atakaewaongoza mtaani kwao. “Sisi ni wanakikundi wa DOTI, tumeanzia kuzunguka maeneo mengi sana katika mitaa ya Dodoma mjini kama Swaswa mnarani, Ntyuka, Nkuhungu Boda, Mwatano na sehemu mbalimbali kwa lengo la kuwahimiza wananchi wajitokeze kupiga kura kwa njia ya maigizo na ngoma” alisema Ramadhani.

Akipongeza juhudi zinazofanywa na Dodoma Jiji Mtaa kwa Mtaa Uchaguzi Festival, mkazi wa Kata ya Ntyuka, Maige Paul, alisema amefurahi ujio wa Mtaa kwa Mtaa Uchaguzi Festival na hiyo inaonesha kwamba wananchi wote tunatakiwa kwenda kuchagua viongozi wanaounda serikali za mitaa akiwemo mwenyekiti na wajumbe wake watano. “Mtaa kwa Mtaa inaendelea kutufurahisha lakini pia inaendelea kutuhamasisha kwamba, jukumu linalofata ni kubwa ambalo tunatakiwa kwenda kuchagua viongozi ambao watatuletea maendeleo katika kata zetu pamoja na mitaa yetu” alisema Paul.




Akiongelea kuhusu wananchi kujitokeza kupiga kura, mkazi wa Kata ya Ntyuka, Latifa Hamadi alitoa rai yake kwa wakina mama na vijana ambao wana sifa za kupiga kura kujitokeza kwa wingi siku ya kuchagua viongozi na kushauri elimu hii isiishie mtaani kwao tu bali ifike na sehemu nyingine. “Nawaomba wakina mama na vijana waliofikisha miaka 18 waende kupiga kura inapofika tarehe 27 Novemba, 2024. Tumependa ujumbe tuliopata katika hamasa hii, lakini pia nawashauri waende kata nyingine nyingi za Jiji la Dodoma kama Kata ya Kilimami, Mkonze na Hazinaalisema Hamadi.

Tamasha la uhamasishaji la Jiji la Dodoma Mtaa kwa Mtaa Uchaguzi Festival linafanywa kwa njia ya kitamaduni na sanaa mbalimbali kwa kutumia maigizo, uchezeshaji ngoma za asili na wasanii nguli wakitumbuiza katika mitaa nyakati za mchana, jioni na usiku  ili kuwafikia wananchi wote wakiwa mitaani kwao na kwa wale wanaoshinda kazini wakirudi waweze kupata burudani pamoja na ujumbe wa elimu ya umuhimu wa kuchagua viogozi watakaoongoza katika mitaa yao.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma