RC Senyamule afafanua uboreshaji daftari la kudumu la wapiga kura

Na. Asteria Frank, DODOMA

 

Mkuu wa Mkoa Dodoma, Rosemary Senyamule ametoa ufafanuzi wa dhana mbalimbali kuhusu uboreshaji wa daftari la kudumu la mpiga kura unaoendelea katika Wilaya ya Dodoma, Chamwino, Bahi na Kongwa.


Mkuu wa Mkoa Dodoma, Rosemary Senyamule


Kauli hiyo aliitoa alipokuwa mbele ya vyombo vya habari leo katika ukumbi wa mkutano ya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa kuhusu juhudi za kuelimisha wananchi wa Mkoa wa Dodoma kuhusu mchakato wa uboreshaji wa daftari la kudumu la mpiga kura unaoendelea katika Wilaya ya Dodoma, Chamwino, Bahi, na Kongwa.

Alisema “napenda kutoa ufafanuzi kuhusu dhana mbalimbali zilizojengeka miongoni mwa wananchi. Kuna taarifa zisizo sahihi zinazozungumziwa kuhusu gharama za uandikishaji, muda wa vitambulisho vya kupiga kura na mchakato wa uboreshaji daftari la kudumu la mpiga kura”.

Aliongeza kuwa uboreshaji taarifa za wapiga kura ni bure, wananchi hawatakiwi kulipa pesa yeyote katika mchakato huo. Dhana ya kwamba  kuna gharama zinazohusiana na uandikishaji ni dhana za uongo na zinapaswa kupuuzwa.

“Pili, vitambulisho vya kupigia kura, tunatoa ufafanuzi kwamba vitambulisho vilivyo tolewa hapo awali ni vitamulisho halali na vinaweza kutumika tena. Hivyo, basi wananchi waliojiandikisha huko nyuma hawapaswi kuhofia kuwa vitambulisho vyao vimekwisha muda wake, na hawahitaji kujiandikisha tena ili wapate vitambulisho vipya. Tatu, kuhusu alama za vidole ni muhimu kujua kwamba wakishachukuliwa alama za vidole hivyo, katika uandikishaji wa awali hawaitaji kuchukuliwa tena, alama za vidole zilizochukuliwa nyuma zilezile zitabaki kuwa halali na zitaendelea kutumika na hii nazungumzia kwa wale wapiga kura waliokuwa halali na hawajabalisha vituo na wala hawana taarifa yeyote ya kubadilisha” alisema Senyamule.

Akitoa ufafanuzi kuhusu uhusiano kati ya uboreshaji wa daftari la kudumu la mpiga kura na uchaguzi wa serikali za mtaa, alisema Mkuu wa Mkoa “mchakato wa uboreshaji wa daftari la kudumu la mpiga kura ni kwaajili ya uchaguzi wa mwaka 2025. Unafanywa kwaajili ya kuhakikisha kuwa kila mtanzania mwenye haki ya kupiga kura, anapata nafasi ya kumchagua diwani, mbunge na rais. Haina uhusiano wa moja kwa moja na uchaguzi wa serikali za mtaa japo tunajua katika mfumo wa uongozi, huu ndio mfumo wa chini wa uongozi kwa nchi yetu. Uchaguzi wa serikali za mtaa una taratibu zake za uandikishaji ambazo zilishatangazwa na waziri mwenye dhamana ya Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa yaani Ofisi ya Rais (TAMISEMI), ambae ni Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa”.

 

Alitoa wito kwa wananchi wote kuwa na uelewa sahihi kuhusu mchakato huo. Alishauri kufuata taratibu zinazotolewa na mamlaka husika ili kuhakikisha wanatimiza haki yao ya kikatiba.

“Na kwamba ili kupata taaria sahihi ama maelezo wanaweza kuwasiliama na viongozi wao wa vitongoji, vijiji, mitaa, kata au waratibu wa uandikishaji ambao wapo kwenye kila halmashauri. Aidha, wanaweza kutembelea tovuti rasmi ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi ambayo ni www.inec.go.tz. Takwimu sawa kuhusu idadi ya wapiga kura Dodoma inakadiriwa kuwa na wapiga kura 1,777,834, kati hao, ambao hawajawahi kujiandikisha kwenye daftari ni 845,976. Aidha, napenda kuwafahamisha wananchi kuwa vituo vya kuandikisha wapiga kura ni vingi. Hivyo, wasiwe na hofu, kwamba watatumia muda wao mrefu vituoni. Katika Wilaya ya Dodoma tuna vituo 429, Wilaya ya Bahi tuna vituo 191, Wilaya ya Kongwa tuna vituo 229 na Wilaya ya Chamwino tuna vituo 805” aliongeza.

 

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma