Magereza wapongezwa kupambana na ukatili wa kijinsia

Na. Valeria Adam, DODOMA

Waziri, Dkt. Gwajima awapongeza wanawake wa Jeshi la Magereza Tanzania kwa kupambana na kuzuia changamoto za ukatili wa kijinsia ili wanawake wachangie katika maendeleo ya taifa.



Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima akifungua mkutano mkuu wa kwanza wa Mtandao wa Wanawake wa Jeshi la Magereza Tanzania


Pongezi hizo zilitolewa na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima alipokuwa akifungua mkutano mkuu wa kwanza wa Mtandao wa Wanawake wa Jeshi la Magereza Tanzania uliofanyika katika ukumbi wa Mtakatifu Peter jijini Dodoma.

“Hatua hii inaonesha ni jinsi gani sera na miongozo mbalimbali ambayo serikali inatoa kuhusu kufikia usawa wa kijinsia katika maeneo mbalimbali nchini, inavyotekelezwa kwa vitendo. Na ninyi mmegeuza miongozo na sera kuwa vitendo kwa kuratibu nchi nzima wanawake katika jeshi hili la Magereza.

Utekelezaji huu ambao umenigusa pia ni kwa sababu una ajenda inayohusu kabisa wizara hii ninayoiongoza ambayo ni ajenda ya kipaumbele ya kupambana na kutokomeza ukatili wa kijinsia, unyanyasaji, udhalilishaji kwa wanawake na watoto katika kazi mbalimbali nchini. Ajenda hii nimeibeba vilivyo na ajenda hii niwaambie kwamba imepokelewa vizuri" alisema Dkt. Gwajima.

Akitoa maelezo ya kina kuhusu mtandao huo kwa mgeni rasmi, Mkuu wa Gereza la Kongwa, SP. Tecla Ngilangwa alisema kuwa mtandao huo umepata mafanikio makubwa. "Dhumuni la mtandao, kwanza ni kuwawezesha wanawake kujitambua, kujiamini, kuthubutu na kujithamini. Pili kuongeza ujuzi na weledi wa wanawake kupitia mafunzo, sekta na makongamano ili waweze kushiriki katika fursa mbalimbali kwa manufaa ya jeshi na jamii. Tatu ni kukuza usawa wa kijinsia na kuimarisha uhusiano kati ya wanawake na mwisho kuhakikisha uwepo wa uwakilishi wa wanawake kiutendaji na kitaalamu ndani na nje ya jeshi kwa kadri inavyowezekana" alisema SP. Ngilangwa.

Aliongeza kwa kusema kwamba mtandao huo haujaweza kufanya kazi kwa ufanisi mkubwa kutokana na changamoto mbalimbali, lakini kuna baadhi ya mafanikio waliyoyapata. “Mafanikio tuliyoyapata ni wanawake kujituma na kufanya kazi kwa bidii na weledi wa hali ya juu. Mengine ni kuongezeka kwa ujasiri kwa watumishi wa kike katika kukabiliana na changamoto zinazowakabili maeneo ya kazi bila kuvunja sheria, kanuni na taratibu za mahali walipo. Pia kuongezeka kwa ari na uthubutu wa kutekeleza majukumu mbalimbali ambayo kabla ya mtandao huu hayakufikiriwa kuwa yanaweza kufanywa na watumishi wa kike kwa ufanisi mkubwa" alifafanua SP. Ngilangwa.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma