KLINIKI YA ARDHI JIJI LA DODOMA YAHUDUMIA WANANCHI 3,056 NDANI YA SIKU 5

Na. Dennis Gondwe, DODOMA

KLINIKI ya Ardhi katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma imehudumia wananchi 3,056 waliokuwa na kero za muda mrefu kuhusiana na sekta ya Ardhi yakiwa ni mafanikio makubwa kwa  wananchi wengi kuhudumiwa kwa muda mfupi.

Mkurugenzi wa Jiji, John Kayombo


Takwimu hiyo ilitolewa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma, John Kayombo alipokuwa akiongea na waandishi wa habari ofisini kwake.

Kayombo alisema “zoezi hili limetoa matokeo chanya kwa ujumla. Wananchi 3,056 walisikilizwa. Hati 1,474 zilitolewa papo hapo. Maombi mapya ya hati 561 yalipokelewa, namba za malipo 1,674 zilitolewa, viwanja 645 vilipandishwa kwenye mfumo, migogoro ya ardhi 774 ilisikilizwa, wananchi 149 walipata huduma za Mipango Miji na wananchi 221 walipata huduma za upimaji” alisema Kayombo.

Akiongelea kliniki hiyo, alisema kuwa ililenga kutatua changamoto za Ardhi kwa haraka. “Zoezi hili ni sehemu ya hatua za utekelezaji wa mkakati wa Mkoa wa Dodoma wa kumaliza changamoto za Ardhi. Kwa mujibu wa mkakati huo zoezi hili nimepangwa kuwa endelevu na litafanyika kwa muda wa wiki moja kwa kila mwezi. Mwezi Oktoba lilianza tarehe 16-20, 2023 katika Ofisi ya Manispaa ya zamani. Aidha, lengo ni zoezi hili kuendeshwa katika ofisi za Tarafa zote nne zilizopo Dodoma” alisema Kayombo.

Mkurugenzi huyo alisema kuwa huduma mbalimbali zinazohusu sekta ya Ardhi zilitolewa. Huduma hizo ni “utoaji wa Hati milki kwa haraka, kusikiliza kero za Ardhi na kuzitafutia ufumbuzi, kutoa elimu ya masuala ya Ardhi pamoja na kurahisisha ulipaji wa kodi ya pango la Ardhi” alisema.

Zoezi la Kliniki ya Ardhi liliandaliwa ma Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maebdeleo ya Makazi kupitia Ofisi ya Ardhi Mkoa kwa lengo la kuwafikia wananchi wenye changamoto za Ardhi katika Jiji la Dodoma kwa kutoa huduma zote za Ardhi katika eneo moja.

MWISHO

 

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma