WAKAZI WA DODOMA WASHAURIWA KUPIMA UDONGO KABLA YA KILIMO

Na. Dennis Gondwe, NZUGUNI

WAKAZI wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma wametakiwa kujenga utamaduni wa kupima afya ya udongo ili kujua mahitaji ya virutubishi kwa udongo vitakavyosaidia kupata mazao mengi na bora.

Mkuu wa Divisheni ya Kilimo Mjini, Yustina Munishi


Kauli hiyo ilitolewa na Mkuu wa Divisheni ya Kilimo mjini katika Halmashauri ya Jiji la Dodoma, Yustina Munishi alipokuwa akiongelea umuhimu wa afya ya udongo kwa mkulima katika kuzalisha mazao bora na yenye tija.

Munishi alisema kuwa kujua afya ya udongo ni muhimu sana kwa mkulima. “Napenda kuwataarifu kuwa kujua afya ya udongo ni muhimu sana kwa mkulima kabla ya kuanza kilimo alichokusudia. Kujua afya ya udongo kunamuwezesha mkulima kujua kiasi cha nyongo au tindikali kilichopo katika udongo. Ukijua afya ya udongo utajua ni zao gani uzalishe na linahitaji virutubisho gani na uweke mbolea ya aina gani na kwa kiasi gani ili uweze kupata mazao yaliyo bora. Hii ni muhimu kwa sababu watu wengi wanadanganyika kwa kuona udongo mweusi anasema hapa kuna mbolea, lakini hatupimi afya ya udongo kwa kuangalia sura na rangi ya udongo. Tumekuja na seti nzima ya upimaji afya ya udogo katika Banda la Halmashauri ya Jiji la Dodoma kwenye maonesho haya ya Nanenane” alisema Munishi.

Nae Emiliana Waitu aliyetembelea banda la maonesho la Halmashauri ya Jiji la Dodoma alisema kuwa amewahi kusikia kuwa udongo huwa unapimwa lakini hakuwa akijua sababu za kupima udongo. “Leo nimeshangaa kuona vifaa vya kupimia udongo na kuelezwa manufaa ya kupima udongo kabla ya kuanza kilimo. Kweli teknolojia imeongezeka na Jiji la Dodoma limetuletea mambo mazuri kwenye maonesho ya Nanenane mwaka huu” alisema Waitu.

Maonesho ya shughuli za wakulima Nanenane mwaka 2023 yanaongozwa na kaulimbiu isemayo “Vijana na wanawake ni msingi imara wa mifumo endelevu ya chakula”.

Baadhi ya wataalam wa Divisheni ya Kilimo mjini wa Halmashauri ya Jiji la Dodoma


MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma