Tofauti kati ya kuboresha taarifa katika daftari la kudumu la mpiga kura na kujiandikisha katika orodha ya wapiga kura

Na. Faraja Mbise, DODOMA


Balozi wa Shina Namba Sita, Mtaa wa Chang’ombe katika Kata ya Ihumwa, Adawila Zakayo alipokuwa akifafanua kwa wananchi tofauti ya zoezi la kuboresha taarifa katika daftari la kudumu la mpiga kura na kujiandikisha katika orodha ya mpiga kura katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa

Zoezi la kuhakiki na kuboresha taarifa katika daftari la kudumu la mpiga kura lililofanyika tarehe 25 Septemba, 2024 hadi Oktoba 1, 2024 lilimtaka mwananchi kwenda kuboresha taarifa zake katika daftari la kudumu la mpiga kura tofauti na zoezi la sasa ambalo linamtaka mwananchi kujiorodhesha katika orodha ya mpiga kura lililoanza tarehe 11 hadi 20 Oktoba, 2024 linalohitaji mwananchi kwenda kuandikishwa kwenye orodha ya mpiga kura kwa lengo mahususi kabisa la kuchagua viongozi  ngazi ya vijiji, vitongoji  na mitaa.

Ufafanuzi huo ulitolewa na Balozi wa Shina Namba Sita, Mtaa wa Chang’ombe katika Kata ya Ihumwa, Adawila Zakayo alipokuwa akifafanua kwa wananchi tofauti ya zoezi la kuboresha taarifa katika daftari la kudumu la mpiga kura na kujiandikisha katika orodha ya mpiga kura katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa.

“Zoezi la kujiandikisha katika daftari la kudumu la mpiga kura lilikuwa ni kwa ajili ya mwakani katika Uchaguzi Mkuu kwa ajili ya kumchagua Diwani, Mbunge na Rais. Hili zoezi la sasa hivi la kujiandikisha katika orodha ya mpiga kura ni kwa ajili ya Uchaguzi wa Serikali za Mtaa ambapo tutamchagua mwenyekiti na wajumbe wake” alifafanua Zakayo.

Alisema kuwa baadhi ya wananchi wamekuwa wakishindwa kutofautisha kati ya kuboresha taarifa na kujiandikisha katika orodha ya mpiga kura. Changamoto hiyo imekuwa ni chanzo cha muitikio mdogo wa watu kujitokeza kwenda kujiandikisha hivyo tunaendelea kutoa ufafanuzi ili kuwasaidia wananchi wetu waweze kujiandikisha katika orodha ya wapiga kura. “Baadhi ya watu wanachanganya juu ya kujiandisha ingawa Tume ya Huru ya Taifa ya Uchaguzi imefanya jitihada kubwa ya kuhabarisha umma kuhusiana na kujiandikisha katika daftari la kudumu la mpiga kura. Watu wengine hawajitokezi kwasababu wanajua zoezi hili linaloedelea la kujiandikisha ni kwa ajili ya kuchukua vitambulisho. Lakini sio, lengo la zoezi hili lililoanza tarehe 11 Oktoba, 2024 ni maalumu kwa kuchagua viongozi wa Serikali za Mitaa” alisema Zakayo.

Hata hivyo, alitoa rai kwa wananchi ambao bado hawajapata uelewa wa matukio haya ya uchaguzi kuwa waendelee kufuatilia vyombo vya habari kwa sababu vinaelimisha kuhusu Uchaguzi wa Serikali za Mitaa na pia waendelee kusikiliza kwa umakini matangazo ambayo yanapita mitaani kwao na kujitokeza kwa wingi kuandikishwa katika orodha ya wapiga kura. “Mimi kama Balozi, nimechukua hatua na kuwahamasisha wananchi kwa kupita nyumba kwa nyumba na kuwatofautishia kati ya zoezi lililopita na hili la sasa la kujiandikisha katika orodha ya wapiga kura. Na pia ninawapigia simu wale ambao nina namba zao nawaambia waende kujiandikisha” alisisitiza Zakayo.

Zoezi lililofanyika Septemba 25 hadi 1 Oktoba, 2024 mwananchi alikuwa na jukumu la kwenda kuboresha taarifa zake kwa yule ambaye amebadili makazi yake na kujiandikisha kwa yule ambaye ametimiza umri wa miaka 18 likiwa maalum kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa madiwani, wabunge na rais. Zoezi linalofanyika hivi sasa la kujiandikisha katika orodha ya mpiga kura lilianza tarehe 11 na litamalizika oktoba 20, 2024 ni kwa ajili ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa ambapo mwananchi anatakiwa kujiandikisha katika eneo lake la makazi ili aweze kumchagua mwenyekiti wa kijiji, kitongoji na wajumbe wa halmashauri.

MWISHO

Comments

Popular Posts

Wananchi Makutupora wafunguka changamoto ya Maji, Umeme na Shule kwa Mkuu wa Mkoa

Waziri Mchengerwa apongeza usimamizi wa miradi jijini Dodoma

Mkataba ujenzi Uwanja wa Mpira wa Miguu wasainiwa Dodoma